YESU NI JIBU

Jumatatu, 28 Desemba 2015

KUWEKEZA KATIKA NDOA NI JAMBO LA MUHIMU SANA LINALOPELEKEA FAMILIA IMARA:


ASKOFU Msaidizi wa Kanisa Katoliki Jimbo la Bukoba, Mhashamu, Methodius Kilaini amewataka wanandoa nchini kuwekeza katika ndoa zao ili kuweza kujenga familia imara.
Askofu Kilaini alisema hayo katika misa ya pili iliyofanyika katika Kanisa Katoliki mjini Bukoba ambapo alisema kuwa bila wanandoa kuwekeza katika ndoa zao, kamwe hawawezi kujenga familia imara.
Alisema Wakristo wanapaswa kujenga tabia ya uvumilivu, upendo, amani, kuthaminiana, kuheshimiana katika familia pamoja na kuombana msamaha kila inapotokea nyufa miongoni mwao.
“Katika suala zima la ndoa inahitaji uvumilivu wa hali ya juu, muwe watu wa kuombana msamaha pindi mmoja wenu anapokosea neno samahani, pole na aksante inapokosekana katika familia zetu, familia haiwezi kuwa imara kwani kila mmoja ataonekana ni mbabe,”alisema.
Alisema ili baba aonekane ni mwenye nyumba anapaswa kufuata utaratibu na kuachana na maisha ya  mwanamume ambaye hajaoa kama vile kuwahi kurudi nyumbani si kila siku kurejea nyumbani kuanzia saa moja hadi usiku wa manane.
“Ukimuoa mwanamke si kwamba ni golikipa tu, iko siku atafungwa goli, kwani mlinda goli hafungwi…. Kuna watu watakufunga tu, … naye  ni binadamu hivyo si vizuri baba mwenye nyumba kurudi kila siku usiku nyumbani,”alisema Askofu Kilaini.
Askofu pia aliwaasa wanawake walioolewa kuwa na adabu kama wake za watu na si kuishi kama wasichana ambao hawajaolewa.
“Katika miaka ya nyuma ilikuwa rahisi kumtofautisha mwanamke aliyeolewa na msichana ambaye bado anatafuta mchumba, lakini siku hizi kuna ugumu fulani, hivyo wanawake mnapaswa kuishi kama mwanamke aliyeolewa pamoja na mavazi yenu,”alisema.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni