YESU NI JIBU

Jumatatu, 22 Septemba 2014

JUHUDI ZA KUPAMBANA NA UGONYWA WA SUKARI:



Wataalamu wa afya wanatahadharisha kuwa juhudi zaidi zinahitajika kupunguza kiwango cha Sukari kinachotumiwa na watu.
Shirika la afya duniani kwa ushirikiano na washauri wa maswala ya afya nchini Uingereza, wamependekeza kupunguza viwango vinavyopendekezwa vya kutumia sukari mwilini.
Ushauri mpya unasema kuwa kiwango kinachostahili cha Sukari mwilini ni asilimia 5 kutoka asilimia 10.
Lakini utafiti mbadala unasema kwamba kiwango kinachofaa hakipaswi kuwa zaidi ya asilimia 3.
Watafiti wanasema kuwa ushauri huu mpya unahitajika ikizingatiwa gharama ya matibabu kwa sekta ya afya hasa matibabu ya magonjwa ya Meno.
Wanasema kuwa Sukari ni kiungo muhimu zaidi katika kuchochea magonjwa ya Meno kwa sababu ya hilo, ni ugonjwa ambao unaweza kuzuilika.
Utafiti unaonyesha kuwa kutumia kiwango kikubwa cha Sukari mwilini kunaongeza uwezekano wa meno kuoza na kuharibika hususan kwa watoto.
Matibabu ya magonjwa ya Meno hugharibu nchi zilizostawi kati ya asilimia 5 na kumi ya matumizi ya pesa za matibabu.
Wataalamu wanasema kuwa hatua zinapaswa kuchukuliwa kwa haraka.
'Kodi kwa Sukari'
Wataalamu wanataka serikali kudhibiti upatikanaji wa mashine za kuuza soda na vinywaji vingine vyenye sukari na hata kuyaondoa katika maeneo ya shule na hospitali.
Pia wanasema kuwa vyakula vyenye kiwango kikubwa cha sukari vinapaswa kuwekwa vibandiko na serikali kuvitoza ushuru mkubwa.
Wanasema kuwa swala la watu kutumia sana Sukari ni tatizo kubwa kwa umma.
Licha ya hatua kuchukuliwa kupunguza matumizi ya Sukari, takwimu zinaonyesha kuwa watu wengi bado wanatumia kiwango kikubwa cha Sukari.

UKIHESHIMIWA HESHIMIKA SEHEMU YA 2


Katika toleo lililopita tulianza mada mpya ya “ukiheshimiwa heshimika” ambapo tulichambua maeneo matatu yaliyojumuisha “Utangulizi”; “Vyanzo vya heshima”; na “Tishio la kujivunjia heshima baada ya kuheshimiwa”! Leo tutaingia katika sehemu muhimu ya sababu kubwa ya kibibilia ambayo husababisha wengi wanaofanikiwa na kuheshimiwa hupoteza heshima zao katika jamii:

Mtazamo wa Yesu kuhusu kujikinai na kuacha kuheshimika

Bwana Yesu aliwahi kuongelea tatizo la hali ya kujikinai baada ya kufanikiwa kiasi cha kudhani mafanikio ni “kibali cha kuishi milele duniani”! Katika kuweka mkazo kuhusu tabia hii, Yesu alitoa mfano wa mtu mmoja tajiri aliyeonesha kujikinai kwa utajiri wake na kutamba kuishi duniani bila ukomo:

“Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.  Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana;  akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu.  Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu.  Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi.  Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani?  Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu. “ (LK. 12:15-21)

Kwa kupitia maandiko haya, unaweza kusoma baadhi ya kauli za tajiri jinsi alivyojikinai akisema: “….ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi…” Kumbuka kwamba huyu tajiri hakuupata utajiri wake kwa njia za ufisadi. Aliupata kwa njia halali kabisaaaa. Alilima shamba lake “likazaa sana…”

Aidha, mpango wa kujenga ghala za kuhifadhi mali zake haukuwa jambo baya hata kidogo! Tatizo lake lilikuwa ni kujikinai, na kujisahau, kwa kufikiri kwamba alifikia kilele cha mafanikio hayo kwa nguvu zake binafsi na kwamba uhai wake utalindwa na wingi wa mali zake!

Ni upumbavu kuacha nyuma mali nyingi
uondokapo badala ya kuzitanguliza uendako


Kutokana na maneno ya Yesu, inaonesha kwamba tabia ya kukusanya na kijilimbikizia mali nyingi kisha ukaondoka na kuziacha bila kuzifaidi ni “Upumbavu”! Kwa mujibu wa maneno ya Yesu ni kwamba upumbavu huu hauishii katika kujilimbikizia peke yake, bali kushindwa kuzitumia mali kwenye mambo ya ufalme wa Mungu; na matokeo yake mhusika kuondoka duniani ghafla na mali zake kuchukuliwa na wengine wasiozitaabikia tangu mwanzo:

“….Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani?  Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu..”

Uchunguzi wangu wa kimaandiko katika mada hii, nimebaini kwamba, kujikinai sio kujisifia utajiri peke yake, wala sio kumsahau Mungu peke yake, bali ni matumizi ya utajiri wenyewe ambayo Yesu amesema kwamba   “….ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu. 

Mambo mawili muhimu hapa. Kwanza, ni tatizo la kujilimbikizia akiba isiyo na matumizi bali imekaa tu kwenye hifadhi yake. Pili, kukataa kutumia akiba ya mali katika vipaumbele vya Mwenyezi Mungu alivyoamuru kwa wale wanaomiliki mali nyingi!

Yesu aliposema “kujitajirisha kwa Mungu” maana yake halisi kwa tafsiri ya toleo la Biblia ya Kiingereza cha Amplified limesema: “So it is with the one who continues to lay up and hoard possessions for himself and is not rich his relation to God…..”  Haya maneno ya “…to lay up and hoard possessions…” yana maana ya kukusanya na kujilimbikizia..” Maana yake na ulimbikizaji ambao matumizi yake hayana mchango wa uhusiano na huduma za kimungu.

Katika uchambuzi huu kuhusu mfano wa Yesu tunajifunza mambo muhimu yafyatayo:
 
1.      Tishio la mali kuchukuliwa na wengine

Mtazamo wa kujilimbikizia mali nyingi ili hatimaye ndipo mkusanyaji apate kuzifaidi hapo baadaye si kitu kipya. Yupo mchaji Mungu aliyepata kuwa tajiri sana kuliko wengi duniani, ambaye alifanya utafiti kuhusu hatma ya utajiri ambapo alihitimisha kwa kusema hayo nayo ni ubatili:

"Nami nikaichukia kazi yangu yote niliyojishughulisha nayo chini ya jua; maana sina budi kumwachia yeye atakayenifuata.  Naye ni nani ajuaye kama huyo atakuwa mwenye hekima au mpumbavu? Hata hivyo atatawala juu ya kazi yangu yote niliyojishughulisha nayo, ambamo ndani yake mimi nimeonyesha hekima chini ya jua. Hayo nayo ni ubatili."(MHU. 2:18, 19)

Kuna maneno haya “……kazi yangu yote niliyojisughulisha nayo chini ya jua,…..” “……..sina budi kumwachia yeye atakayenifuata…….” “…… atatawala juu ya kazi yangu yote niliyojishughulisha nayo…….” hayo nayo ni ubatili.”

Aliyeandika haya ni mfalme Sulemani ambaye alijikusanyia mali na utajiri mwingi kuliko matajiri wote wa ulimwengu waliowahi kuwepo kabla na baada yake. Ushahidi mwingine wa utafiti wa Mhubiri unapatikana katika maandiko yafuatayo:

“Maana kuna mtu ambaye kazi yake ni kwa hekima, na kwa maarifa, na kwa ustadi; naye atamwachia mtu asiyeshughulika nayo kuwa sehemu yake. Hayo tena ni ubatili, nayo ni baa kuu.” (MHU. 2:21)

Katika maandiko haya tunakutana na maneno haya.. “….Mtu ambaye kazi yake ni kwa hekima, na maarifa, na kwa ustadi….” “…….naye atamwachia mtu asiyeshughulika nayo kuwa sehemu yake…”

Hili jambo lilimchanganya sana Sulemani. Mtu anakusanya mali nyingi kwa muda mrefu na nguvu nyingi, akisha kufikia kilele cha ulimbikizaji kabla hajazifaidi anaondoka ghafla, na mtu mwingine anazichukua bila kuzitaabikia!!

2.      Kufananishwa na Mpumbavu

Yesu anamtaja tajiri Yule kuwa “Mpumbavu”! Ukifuatilia kwa makini Bibilia inamtafsiri “mpumbavu” ni mtu yeyote asiyetambua uwepo wa Mungu:

“Mpumbavu amesema moyoni, hakuna Mungu; wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, hakuna atendaye mema.” (Zab.14:1)

Hivi ndivyo Yule tajiri mkulima alivyoonnesha upumbavu wake ambapo Yesu aliutafsiri kwamba ni “dhana potofu ya uzima wa mtu kuwa katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo..”

3.      Jinsi ya kuweka akiba yenye tija ya milele

Haya basi, baada ya kuuthibitisha hasara ya kujilimbikizia mali na kisha kufa ukaziacha na kuondoka patupu, Yesu alipendekeza njia ya kunufaika na mali za duniani hata baada ya kuondoka duniani ni kuhakikisha matumizi ya mali hizo yanatoa kipaumbele kwa mambo ya ufalme wa Mbinguni:

“Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi hujunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.” (Mat.6:19-21)

Katika maandiko haya, ukiyatafsiri kwa mtazamo wa mfano wa tajiri aliyejilimbikizia mali kibinafsi, utagundua maana kama ifuatavyo: Kwanza, kukusanya mali na kuzitumia kwenye mambo ya ufalme wa Mungu ndiyo njia pekee ya kulimbikiza mali mahali salama kwa maana kwamba mali zinakutangulia uendako badala ya kuziacha nyuma yako uondokapo.

Majumuisho kuhusu kujikinai na kupoteza heshima

Watu wengi hutumia nguvu na muda mwingi katika kutafuta mafanikio kwa njia mbali mbali. Baada ya kufikia mafanikio na wahusika kupata kutambuliwa, na kupata umaarufu na heshima kutokana na mafanikio waliyoyapata, ghafla hubadilika kitabia na kupotesha heshima ile ile waliyokuwa wameipata kutokana na kazi kubwa waliyokwisha kuifanya.

Moja wapo ya tabia mbaya inayopoteza heshima ni kujikinai na kudhani kwamba, mafanikio hayo ni juhudi binafsi na Mungu hana sehemu wala jamii inayowazunguka. Kimsingi hakuna mtu afanikiwaye yeye peke yake kwa juhudu zake binafsi, pasipo ridhaa ya Mungu, na pasipo mikono ya watu wengine kuhusika kwa njia moja au nyingine. Hata kama maono, mipango na mikakati ya utekelezaji imebuniwa na mtu mmoja; bado ufanisi wake lazima hujumuisha wengi hata kama waliohusika walifanya hivyo kwa malipo.

Aidha, ni upumbavu wa hali ya juu, pale ambapo mtu afikiapo mafanikio ya kiuchumi, kufikiri kwamba ataishi milele duniani ili kunufaika kibinafsi na utajiri aliojilimbikizia hapa duniani. Tunao ushahidi wa maelfu ya watu wengi ambao kwa muda fulani walifanikiwa katika kumiliki uchumi na kupata umaarufu lakinii ghafla wahusika wakatoweka ghafla kwa maradhi yaliyooshindikana kutibika japokuwa walikuwa na mali nyingi. Mali zile hazikuwasaidia kudhibiti na kurefusha maisha yao, wakaondoka pasipo kutaka.

Kana kwamba hii haitoshi, watu wengi waliojilimbikizia mali nyingi, wanapoondoka ghafla haichukui muda mrefu hata na mali zile walizohifadhi huangukia mikononi mwa watumiaji wasio na uchungu nazo, na kisha kutoweka na kubaki historia tu.

Matokeo haya, ya kujikinai na kuishia kupoteza heshima ni changamoto kwa jamii ya kizazi cha wanaofanikiwa katika karne hii ya ishirini na moja. Katika toleo lijalo tutapitia kwa kina matumizi mabaya ya mali na utajiri na athari zake kwa wahusika pamoja na jamii kwa jumla.

Itaendelea toleo lijalo

MAOMBI YA UREJESHO NA UKOMBOZI SEHEMU YA PILI MGUSO WA PILI (Second touch)

TOKA NDANI YA KABURI, FUNGUA SANDA ILI UWEZE KUSTAWISHWA.

Wiki jana nilikufundisha ni kwa namna gani BWANA anaweza kukugusa kwa mara ya pili na nilikutolea mfano juu ya yule mtoto wa mwanamke Mshunami ambaye alikuwa ndani ya jeneza tayari kwa kwenda kuzikwa lakini BWANA awezaye kutenda miujiza aliligusa jeneza na kumwambia kijana amka na ikawa hivyo.
Bado naendelea na somo hili na leo utakwenda kuangalia na  mfano wa mtumishi wa Mungu Lazaro, endelea...
Neno la Mungu linasema, “Basi mtu mmoja alikuwa hawezi  Lazaro wa Bethania, mwenyeji wa mji wa Mariamu na Martha, dada yake.Ndiye Mariamu yule aliyempaka Bwana marhamu, akamfuta miguu kwa nywele zake ambaye Lazaro nduguye alikuwa hawezi. Basi wale maumbu wakatuma ujumbe kwake wakisema Bwana, yeye umpendaye hawezi. Naye Yesu aliposikia  alisema, Ugonjwa huu si wa mauti bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo. Naye Yesu alimpenda Martha na umbu lake na Lazaro. Basi aliposikia ya kwamba hawezi alikaa bado siku mbili pale pale alipokuwapo. Kisha baada ya hayo akawaambia wanafunzi wake, Twendeni Uyahudi tena.Wale wanafunzi wakamwambia Rabi juzijuzi tu Wayahudi walikuwa wakitafuta kukupiga kwa mawe nawe unakwenda huko tena?Yesu akajibu, Je! Saa za mchana si kumi na mbili? Mtu akienda mchana hajikwai; kwa sababu aiona nuru ya ulimwengu huu.Bali akienda usiku hujikwaa; kwa sababu nuru haimo ndani yake.Aliyasema hayo; kisha, baada ya hayo akawaambia Rafiki yetu Lazaro amelala lakini ninakwenda nipate kumwamsha.Basi wale wanafunzi wakamwambia Bwana ikiwa amelala atapona.Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi Lazaro amekufa.Nami nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwako huko, ili mpate kuamini; lakini na twendeni kwake.....Basi Yesu alipofika alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne.Na Bethania ilikuwa karibu na Yerusalemu kadiri ya maili mbili hivi na watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao. Basi Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alikwenda kumlaki; na Mariamu alikuwa akikaa nyumbani.Basi Martha akamwambia Yesu Bwana kama ungalikuwapo hapa ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa.Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka.Martha akamwambia najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.Yesu akamwambia mimi ndimi huo ufufuo na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi;naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu yule ajaye ulimwenguni.....Bali wengine wao wakasema, Je! Huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife?Basi Yesu hali akiugua tena nafsini mwake, akafika kwenye kaburi. Nalo lilikuwa ni pango na jiwe limewekwa juu yake.Yesu akasema liondoeni jiwe. Martha dada yake yule aliyefariki, akamwambia Bwana ananuka sasa maana amekuwa maiti siku nne.Yesu akamwambia, Mimi sikukuambia ya kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu, akasema Baba nakushukuru kwa kuwa umenisikia.Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia sikuzote lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma. Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa amefungwa sanda miguuni na mikononi na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake. Basi wengi katika Wayahudi waliokuja kwa Mariamu na kuyaona yale aliyoyafanya wakamwamini.Lakini wengine wakaenda zao kwa Mafarisayo wakawaambia aliyoyafanya Yesu” Yohana 11:1-46
 Ni dhahiri kuwa vipo vifungo vingi vinavyofuata maisha ya watu wa Mungu waliokoka na vimekuwa vikwazo vizito ambavyo vinahitaji mguso wa pili ili vitoke.
MGUSO WA KWANZA
Katika mguso wa kwanza tunaona jinsi Yesu alivyomfufua Lazaro kutoka  kaburini maana Yesu Kristo yeye ndiye mwenye funguo za mauti na kuzimu sawa na neno hili, “Na aliye hai nami nalikuwa nimekufa na tazama  ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu. Ufunuo 1:18
 Yesu Kristo  anafunguo za mauti na kuzimu na ndio maana  aliweza kumfungua Lazaro toka katika kaburi na mauti maana ni ahadi yake, “Nitawakomboa na nguvu za kaburi nitawaokoa na mauti ewe mauti, ya wapi mapigo yako? Ewe kaburi, ku wapi kuharibu kwako? Kujuta kutafichwa na macho yangu” Hosea 13:14
Yesu Kristo alipofika kaburini alimwita  Lazaro na kumwambia  atoke nje na mara Lazaro akatoka nje  yule aliyekuwa amekufa  yapata siku nne. Hivyo hata kama biashara, kazi na elimu yako  zimekufa leo zitafufuka maana mwenye funguo yupo tayari kukugusa.
MGUSO WA PILI
Katika mguso wa pili tunaona  mara baada ya kumwambia Lazaro atoke nje akawaambia wamfungue sanda alizokuwa amefungwa na wamuache aende zake, “Akatoka nje yule aliyekufa amefungwa sanda miguuni na mikononi na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia mfungueni, mkamwache aende zake”
Hivyo ni dhahiri kuwa BWANA atakuinua tena hata kama walikuangusha ili wapate  kukuangamiza huu ni wakati wako wa kuinuliwa ,” Hapo watakapokuangusha utasema, kuna kuinuka tena naye mnyenyekevu Mungu atamwokoa” Ayubu 22:29
BWANA  anasema huu ni wakati wa kuinuka kiroho na kimwili ,baraka zako lazima ziinuke na ustawi wako lazima uinuke mali na zako pia.“Nami nitakatilia mbali uchawi  usiwe mkononi mwako wala hutakuwa tena na watu wenye kutabana” Mika 5:12
Kama ambavyo sanda ya Lazaro ilivyofunguliwa ndivyo sanda ya uchawi na mikosi iliyofunga  mikono yako isishike pesa, biashara yako isifanikiwe itakatiliwa mbali na ndipo utakapo stawishwa tena .
BWANA  anasema nitakufungua na nitakuacha  uende zako  na wao waliokushusha,waliokufilisi, waliosema hautaolewa, waliosema hautazaa wala hutofauli masomo  yako nawaambia ya kuwa  mimi  BWANA Mungu wako nitakutoa nje na kukufungua hayo yote.
Kama ambavyo Yesu Kristo alisema Lazaro toka nje  ndivyo nasi leo tutakavyomwita Lazaro wetu atoke nje na akisha tumfungue sanda.
“Siku hiyo nitaiinua tena maskani ya Daudi iliyoanguka na kuziba mahali palipobomoka nami nitayainua magofu yake, na kuyajenga kama siku za kale” Amosi 9:11
BWANA  anataka tuinuke kiroho na kiuchumi na miguu iliyofungwa tuifungue kwa jina lake kama ambavyo  Lazaro alifungwa mikono, miguu na uso kwa sanda na ilikuwa na maana ya kuwa  pamoja na kufufuka bado asingeweza kutembea na kwenda popote maana amefungwa sanda.
Hivyo maisha ya Lazaro yakawa giza wala haoni mbele hivyo basi hata sisi yatupasa tufungue sanda zote ili  maisha yetu yatiwe  nuru.
“Mwenye haki atasitawi kama mtende  atakua kama mwerezi wa Lebanoni. Waliopandwa katika nyumba ya Bwana watasitawi katika nyua za Mungu wetu. Watazaa matunda hadi wakati wa uzee, watajaa utomvu  watakuwa na ubichi” Zaburi 92:12-14
Yakupasa  usiogope wala kufadhaika maana upo  mguso wa pili na  utarejeshewa upya, “Utukufu wangu utakuwa mpya kwangu, na uta wangu hurejezwa upya mkononi mwangu”Ayubu 29:20
Pia hapatakuwapo na utasa katika nyumba yako,  Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba wala aliye tasa katika nchi yako na hesabu ya siku zako nitaitimiza” Kutoka 23:26
Magonjwa hayatainuka kwako , Nanyi mtamtumikia Bwana Mungu wenu naye atakibarikia chakula chako na maji yako nami nitakuondolea ugonjwa kati yako” Kutoka 23:25
Wachawina tunguli zao hawatakupata maana,  “Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo wala hapana uganga juu ya Israeli. Sasa habari za Yakobo na Israeli zitasemwa, ni mambo gani aliyoyatenda Mungu! “ Hesabu 23:23



Bwana amenipa funguo lazima ufunguliwe katika mguso wa pili.“Na ufunguo wa nyumba ya Daudi nitauweka begani mwake  yeye atafungua wala hapana atakayefunga naye atafunga wala hapana atakayefungua” Isaya 22:22
Ni wazi kuwa huu ni wakati wa kuinuliwa lazima uinuke na ufungue  sanda katika kazi zako,ndoa yako na unatakiwa kusimama mwenyewe katika zamu yako kama ambavyo Isaka alisimama na kumlilia Mungu juu ya Rebeka mkewe na akapata mtoto, “Isaka akamwomba Bwana kwa ajili ya mke wake, maana alikuwa tasa. Naye Bwana akamwitikia na Rebeka mkewe akachukua mimba”Mwanzo 25:21.
Hivyo maneno haya yafanyike chachu katika maisha yako na unapaswa kusimama uombe mbele za Mungu naye atakuitikia na sanda zote zitakuachia.

Jumamosi, 20 Septemba 2014

WITO WATOLEWA KWA WATU WA DINI ZOTE KUHUDHURIA MAOMBI NA MAOMBEZI KATIKA VIWANJA VYA SIFA ZA YESU MANZESE JIJINI DAR ES SALAAM:



Imeelezwa kuwa ni vyema  watu kusimama na kumtumikia Mungu na kufuata taratibu na miongozo ya Kimungu ili waweze kuondokana na mateso ,taabu na shida mbalimbali zinazo wakumba katika maisha ya kila siku.
Wito huo umetolewa na mtumishi wa MUNGU mchungaji Paul Kaisi wa huduma ya Liko Tumaini Kwa Mungu ilipo katika Viwanja vya sifa za Yesu Manzese jijini DSM.
Ametoa wito huo wakati akifundisha neno la MUNGU na kusema watu wenye matatizo mbalimbali na kufungwa na dhambi kujitokeza kuhudhuria ibada hiyo kwa lengo la kufunguliwa na kuacha dhambi.
Aidha alisema kuwa watu wengi wamefungwa bila kujua na adui hivyo ni muhimu kuhudhuria ibada hiyo ya kufunguliwa siku ya jumapili hii kuanzia saa tatu kamili na kuendelea na maombi na maombezi yatafanyika kwa kila atakayehudhuria.

Jumanne, 16 Septemba 2014

JENGO LA GHOROFA TANO MALI YA KANISA LA SCOAN LAPOROMOKA.



Idadi ya watu waliokufa kwenye ghorofa la makao makuu ya Kanisa la SCOAN (Synagogue Church of All Nations) la Nabii TB Joshua wamefikia 50.
Jengo hilo la ghorofa tano ambalo ni makao makuu ya kanisa na nyumba ya kulala wageni liliporomoka Jumamosi  wakati ujenzi ukiendelea.
Hadi kufikia siku ya  Jumapili jumla ya watu 41 walikuwa wameripotiwa kufa,lakini maiti nyingine tisa zimeongezeka.
Inaelezwa kwamba,mhubiri huyo wa kimataifa alipewa kibali cha kujenga ghorofa mbili,lakini mwenyewe akaamua kujenga ghorofa tano.
Uokoaji bado unaendelea na watu wengine mia moja na ishirini na nne walikuwa wameokolewa wakiwa hai hadi kufikia siku ya jumapili.
 Kiongozi wa kanisa la Synagogue Church of All Nations(SCOAN) Nabii TB Joshua nyuma ni jengo liloporomoka

Baadhi ya majeruhi waliookolewa kwenye kanisa hilo akiwa hajitambui.


 Waokoaji wakienddelea na shughuli za uokoaji.
 Picha hizi ni kwa idhini ya premiumt times -Micheal Abimboye,