Ofisa
Mipango Mwandamizi wa Internews, Victoria Rowan akito mada katika mafunzo kwa
wanadishi wa habari kuhusu usawa wa kijinsia.
NA MWANDISHI WETU
MHADHIRI Msaidizi wa Shule Kuu ya
Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma (SJMC) Zuhura Selemani, amesema
vyombo vingi vya habari vinaandika na kutangaza habari zinazowahusu wanaume
kuliko wanawake jambo ambalo si sawa.
Katika mada yake kwa wanahabari katika
mafunzo ya siku moja kuhusu usawa wa kijinsia hususan katika siasa na uongozi
pamoja na nafasi ya wanwake katika vyombo vya habari, Zuhura amenukuu utafiti
uliofanywa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) mwaka 2019, akisema ingawa
wanawake wengi huhitimu katika vyuo na vyuo vikuu vya uandishi wa habari kuliko
wanaume, bado idadi ya wandishi wa habari wanawake katika vyombo vya habari na
taasisi nyingine ni ndogo kuliko wanaume.
“Vyombo vingi vya habari pia
havina sera kuhusu masuala ya jinsia na vingi kati ya vilivyo na sera hizo,
havizitumii,” alisema.
Katika mafunzo hayo
yaliyoandaliwa na taasisi ya Internews kupitia mradi wa Boresha Habari,
Msimamizi wa Vyombo vya Habari wa Internews, Alakok Mayombo, alisema vyombo vya
habari vinapaswa kuonesha mfano bora kwa kuandika na kutangaza habari kwa
kuzingatia usawa wa kijinsia kwa kupaza sauti za watu walio katika makundi
maalumu wakiwamo wanawake na wenye ulemavu.
Alisema ukosefu wa usawa wa
kijinsia bado ni tatizo kubwa katika jamii katika nyanja mbalimbali zikiwamo za
siasa, uwakilishi na uongozi sambamba na nafasi katika vyombo vya habari.
“Bado tatizo hili ni kubwa hivyo,
lazima wanawake na wanaume washirikiane kuliondoa maana tunataka wote wasonge
mbele hata katika shughuli zenye changamoto ili wapate uzoefu na nafasi ya
kupanda juu hata katika vyombo vya habari hivyo, lazima hata wanaume
waelimishwe na kushirikishwa katika juhudi hizi ili washiriki kuleta mabadiliko
badala ya kuwa watazamaji,” alisema Alakok.
Mtaalamu huyo wa habari alisema
lengo la kufikia uwiano wa 50 kwa 50 halipaswi kuwa katika siasa pekee, bali
pia katika taaluma mbalimbali ikiwamo ya habari kwa kutoa nafasi sawa kwa
wanawake na wanaume.
“Sauti za wanawake zisikike na
pia, ni vema zioneshe mafanikio na uwezo wao badala ya wanawake kuoneshwa tu
kwa matukio mabaya kama ya kubakwa na kupigwa,” alisema.
Katika mada yake iliyosisitiza
tofauti baina ya jinsi na jinsia, Ofisa Mipango Mwandamizi wa Internews,
Victoria Rowan, alisema ili kufikia usawa wa kijinsia, lazima wanawake na watu
wenye ulemavu wapewe nyenzo na kusaidiwa kwa hali na mali ili kufikia uwiano.
“Si tu suala la wote kupata kwa
usawa, bali walio pembezoni wapewe nguvu zaidi ili wafikie wenzao katika nyanja
mbalimbali kama siasa, uongozi na kiuchumi kwa kuwa hakuna anayezaliwa akiwa
kiongozi, bali wote huandaliwa,” alisema Rowan.
Alisema wanawake hawana budi
kujengewa uwezo wa kujitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ukiwamo wa
kisiasa huku kukiwa na mazingira wezeshi kama usalama, elimu na nguvu za
kiuchumi.
Aliwataka wanawake kutojiweka
nyuma zinapotokea fursa mbalimbali, bali wajitokeze na kuzichangamkia.
Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi
isiyo ya kiserikali inayobadilisha maisha ya wanawake vijana na watoto (TIBA),
Marcela Lungu, alisema elimu sahihi na endelevu inapaswa kutolewa kwa
jamii ili kufikia usawa wa kijinsia.
Marcela alisema, “Vyombo vya
habari vioneshe nguvu ya wanawake katika jamii ili jamii iwaone na kuwapa
nafasi maana wapo wanawake wengi wenye uwezo mkubwa wa uongozi, lakini hawapati
nafasi.
Akaongeza, “Tatizo hili
linachangiwa pia na mtazamo hasi wa jamii, baadhi ya mila na desturi na baadhi
yao wenyewe kutojiamini.”
Akijikita katika nadharia za
uongozi katika mtazamo wa jinsia, mtaalamu wa masuala ya jinsia na maendeleo,
Michael Marwa, alisema kitendo cha wanawake kujifunza majukumu yao mengi wakiwa
katika umri mdogo, huathiri mitazamo yao na uchaguzi wa shughuli zao za
kimaisha.
“Hili ndilo husababisha mtazamo
kuwa jamii au kundi fulani ni viongozi bora kuliko wengine katika jamii jambo
ambalo si kweli,” alisema.
Marwa ambaye pia ni Mkuu wa
Mipango katika taasisi ya C-SEMA mkoani Dar es Salaam, alisema ukosefu wa
uwakilishi wa kutosha wa wanawake katika uongozi si matokeo ya kinachodaiwa na
baadhi ya watu kuwa uwezo mdogo au wanawake kutojiamini, bali imani potofu kuwa
wanawake hawawezi kuwa viongozi bora.
“Jamii inapaswa kubadili mitazamo yao na kuweka usawa baina ya wanawake na wanaume,” alisema Marwa.