YESU NI JIBU

Alhamisi, 5 Machi 2015

VOINGOZI WA DINI KUSIMAMA NA KUKEMEA KWA SALA WALE WANAOJIHUSISHA NA UJANGILIWA WANYAMAPORI NCHINI.




Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, amewataka viongozi wa dini kuwakemea kwa sala watu wanaojihusisha na ujangili kwenye hifadhi za wanyamapori nchini, ili waachane na vitendo hivyo.
Nyalandu alitoa wito huo jana wakati akizungumza na viongozi hao kwenye ziara yao ya kutembelea hifadhi ya wanyamapori ya Tarangire mkoani hapa, iliyoandaliwa na wizara yake kwa kushirikiana na taasisi ya kimataifa ya kupambana na mauaji ya wanyamapori na biashara ya pembe za ndovu na faru ya Wild Aid.
Alisema wizara yake imeamua kuwashirikisha wadau wote katika vita dhidi ya ujangili wa wanyamapori wakiwamo tembo na faru.
“Nawaomba viongozi wa dini muwakemee kwa sala wale wote wanaoua wanyama wetu, waelezeni faida za wanyama hawa kwa taifa ili waache vitendo hivi viovu haraka sana, ” alisisitiza Nyalandu.
Kwa upande wao, viongozi hao  wameitaka serikali kuweka sheria kali katika uhifadhi wa wanyama pori na mazingira ili kutokomeza  uwindaji haramu wakiwamo tembo na faru.
Askofu wa Kanisa la Anglikana, Dk.  Valentino Mokiwa,  alisema viongozi wa dini wana  uwezo mkubwa wa kueneza taarifa za kupiga vita mauaji ya tembo kwa kuwaonya na kuwaelekeza waumini katika misikiti na makanisa.
Aliitaka serikali kutazama kwa kina utalii wa uwindaji ili kuona kama ndiyo kichocheo cha mauaji ya tembo ili kuendelea kuhifadhi wanyama pori.
Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam,  Alhad Salum,  alisema amefurahishwa na wizara hiyo kuwapa fursa ya kuangalia wanyama katika hifadhi hiyo kwa sababu imewasaidia kufahamu maisha yao, hivyo atahamasisha waumini kuungana kupiga vita ujangili.
Mwakilishi wa Jumuiya za Kikristo Tanzania, Mchungaji Grace Masakulangwa, aliitaka serikali kutokomeza mtandao wa biashara ya pembe za ndovu nchini.
“Serikali inafahamu mtandao wa wahalifu hawa wanaotumalizia wanyama. Ilivunje genge la watu hao haraka  kwani  vyombo vya ulinzi na usalama vina taarifa zao, ” alisema Masakulangwa.
Nabii Askofu, Ephata Mwingira, alisema serikali imefanya jambo jema kuwashirikisha na kuwataka viongozi wake  waonyeshe dhamira ya kweli katika mapambano ya kulinda rasilimali.
Je wewe unamaoni gani kwa hili ambalo viongozi wa dini kuombwa kukemea majangili kwa sala. 

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni