Jumapili
iliyopita tulifanya uchambuzi wa fungu
la karama za mafunuo ambazo ni neno la hekima, neno la maarifa, na kupambanua
roho. Leo tunaanza fungu jipya la karama za NGUVU ambazo ni Imani, karama za kuponya
magonjwa, na karama ya matendo ya miujiza.
Karama ya Imani
Awali ya yote, kabla sijaichambua karama ya imani, hebu
nitoe tafsiri fupi ya msamiati wa neno imani kibiblia ina maana gani. Imani ni
"hisia ya rohoni ya kuwa na hakika na mambo ya ki-Mungu zikiwemo ahadi
zake pamoja na kutambua uwepo wake kama Mungu Muumbaji na mwenye uwezo wote,
asiyeshindwa lo lote na yuko mahali pote na anajua mambo yote.
Kitabu cha Waebrania kimeandika kwamba: "Basi,
imani ni KUWA na hakika ya mambo yatarajiwayo, na bayana ya mambo yasiyoonekana
bado." (EBR 11:1)
Imani hii chanzo chake ni Injili ya wokovu inapohubiriwa
kwa mwenye dhambi, akaisikia ndipo hushawishika na kuanza KUWA na hakika ya
ukombozi wa Yesu Kristo. Kitabu cha Warumi kimeandika chimbuko la Imani kuwa: "chanzo
cha imani ni kusikia, na kusikia kunatokana na Neno la Kristo."
(Rum.10:17)
Kila mwamini aliyeokoka anayo imani ya Kristo. Kwa imani
hiyo, amepokea wokovu na kuhesabiwa haki mbele za Mungu. Haya sasa tuje
kwenye tafsiri ya karama ya Imani kama ifuatavyo:
Karama ya Imani ni uwezo maalum wa Roho Mtakatifu
unaoshukia au kujazwa ndani ya mtu ambaye amejaliwa/kutumiwa na Roho kwa ajili
ya kufanya jambo/tendo kubwa ambalo liko nje ya uwezo wa kawaida wa
kibinadamu. Karama ya Imani ni uwezo maalum wa KUWA na hakika/ujasiri wa
kuchukua hatua kufanya jambo ambalo linahitaji uwezo kutoka kwa Mungu peke yake
ndipo lifanikiwe
Karama ya imani humwezesha mhusika kukabiliana na
changamoto au upinzani mkali na akamudu kushinda wakati waamini wengine
wamekata tamaa kabisa. Karama ya imani ni moja ya karama za nguvu ambayo
pia huzichochea zile karama za kuponya magonjwa na matendo ya miujiza kutenda
kazi zake.
Na pia ili karama nyingine ziweze kufanya kazi lazima
karama ya Imani imwingie muhusika na kumpa uwezo wa kutumiwa kwenye maeneo
mengine. Kwa mfano kitendo cha Yesu kutembea juu ya maji kilihusisha karama
mbili mojawapo ikiwa ni karama ya imani.
Kitendo cha kufufua wafu kilihusisha karama mbili ikiwemo
karama ya Imani. Kitendo cha Yesu kubariki mikate michache wakala watu zaidi ya
elfu tano kilihusisha karama mbili mojawapo ikiwa ni karama ya Imani. Kwa hiyo
karama ya Imani ni kama ufunguo wa utendaji wa fungu la karama za NGUVU.
Hapo awali nilisema kila mwamini Aliyezaliwa mara ya pili
anayo imani ambayo ndiyo ilimwezesha kupokea wokovu na baraka za kiroho. Kwa
imani hiyo mwamini anahesabiwa haki mbele za Mungu. Lakini si kila mwamini
ambaye anaweza kutumiwa na Karama ya Imani.
Karama za
kuponya magonjwa
Jana tulianza kulichambua fungu la karama za nguvu ambazo
nj Imani, karama za kuponya magonjwa na karama ya matendo ya miujiza: na
tukapata kuichambua karama ya imani Leo nataka tuchambue karama ya pili, ambayo
ni karama za kuponya magonjwa. Kabla ya yote nitoe maelezo ya msingi
kuhusu suala zima la uponyaji wa magonjwa.
Kuna tofauti kubwa kati ya uponyaji na tiba. Tiba ni
inahusiana na matumizi ya dawa katika kutibu magonjwa. Uponyaji ni uwezo wa
kuondoa magonjwa au kurejesha afya njema pasipo matumizi ya dawa au lishe
maalum.
Ni kutokana na aina hii ya uwezo wa kuondoa maradhi au
magonjwa katika mwili wa binadamu na akarejea kwenye afya njema, akawa mzima
inaleta msamiati wa kibiblia wa "Karama za kuponya magonjwa"!
Yesu Kristo ndiye mwanzilishi wa huduma za kuponya
magonjwa na akiwa ndiye Mponyaji Mkuu wa magonjwa yote. Aidha, ni Yesu ALIYETOA
mamlaka kwa wanafunzi wake wanapotangaza Injili yake wafanye maombezi ya
kuponya magonjwa.
Sasa tuje kwenye utendaji wa hii karama za kuponya
magonjwa. Hii inaitwa karama za kuponya magonjwa katika wingi badala ya umoja.
Maana yake karama za kuponya ziko zaidi ya karama moja. Hizi karama za
kuponya magonjwa ziko katika wingi kwa sababu na magonjwa yako ya aina nyingi
pia. Kwa mantiki hii kila aina ya ugonjwa ipo karama maalum ya kuushughulikia.
Lakini pia karama za kuponya ziko katika wingi kwa maana
kwamba, Roho Mtakatifu huzigawa karama za kuponya kwa waamini tofauti tofauti
badala ya mwamini mmoja kutumiwa katika karama za kuponya magonjwa
yote. Wako waamini wanaotumiwa kuponya aina fulani ya magonjwa, au kuponya
baadhi ya magonjwa na sio magonjwa yote.
Huu ni mgawanyo wa Roho Mtakatifu akitaka kuwatumia
waamini tofauti ili kudhibiti mtu mmoja kuhodhi kila karama kwa magonjwa yote.
Karama ya
matendo ya miujiza
Karama ya matendo ya miujiza maana yake ni uwezo wa kiungu
wa kufanya mambo ambayo yako katika uwezo wa asili wa kibinadamu. Kwenye karama
ya miujiza kama jina lake lilivyo kazi yake kufanya mambo ya kushangaza na
kutisha yaliyoko nje ya uwezo wa kanuni za asili. Maana ndani ya karama ya miujiza
ndimo ulimo uwezo wa uumbaji wa kimungu. Mathalan, Yesu kutungwa mimba kwa
uwezo wa Roho Mtakatifu ni karama ya matendo ya miujiza.
Huko nyuma nimeeleza kwamba karama ya kutenda miujiza
hufanya kazi bega kwa bega na “karama ya Imani” maana zinategemeana sana,
tofauti na karama za kuponya magonjwa. Karama ya matendo ya miujiza inahusisha
matendo yote kuanzia kurejesha upya viungo vya mwili vilivyoharibika mpaka
uwezeshaji wa vitu chache kutosheleza mahitaji makubwa kuliko uwezo wake wa
kawaida.
Kwa kupitia karama ya miujiza, Roho Mtakatifu ndani ya
mwamini anaweza kumtumia kufanya jambo ambalo ni la kushangaza na waisoamini
wakamtukuza Mungu kwa ajili ya tukio hilo.
Naomba kutoa tahadhari hapa kwamba, kuna vituko vingi siku
hizi katika huduma za kimaombezi ambavyo vinaitwa miujiza lakini sio utendaji
wa “karama ya miujiza”. Mfano vitendo vya watu kuanguka chini kwa mkupuo vinatafsiriwa
kuwa ni “karama ya miujiza” wakati ukweli sio.
Ni kweli kwamba Inashangaza kwa macho! Shetani naye
anaweza kuangusha watu saaana tu. Sasa kitu ambacho Ibilisi anaweza kukitumia
kwa urahisi kudanganya watu kama kiini macho au mazingaombwe hakiwezi kutafsiri
kuwa hiyo ni karama ya miujiza inayotendwa na Roho Mtakatifu.
Karama ya miujiza hutenda jambo ambalo Ibilisi hawezi
kuigiza au kulifanya kwenye mazingira ambayo Roho Mtakatifu anatawala.
Kwa mfano watumishi wa Ibilisi nao wanaweza wakacheza na
mapepo kwenye mikutano ya hadhara, lakini sio kwamba huwa wanatoa pepo. Wao
“wanapunga pepo” badala ya “kutoa pepo”. Lakini matukio yote yanahusisha
udhuhuriko wa mapepo. Hapa ndipo inahitaji ile “Karama ya kupambanua roho” ili
kutofautisha muujiza wa Roho Mtakatifu na mazingaombwe na viini macho vya
Ibilisi.
Itaendelea
toleo lijalo
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni