YESU NI JIBU

Alhamisi, 9 Oktoba 2014

KUTOKUJIHESHIMU HUZAA KUTOKUHESHIMIKA:


Kutokujiheshimu ni kupunguza au kuacha kabisa kufanya mambo yale yaliyokufanya uheshimike.

Kufanya mambo kinyume na matarajio ya wale waliokuwa wanakuheshimu.
Mara nyingi watu wakutanapo kwa mara ya kwanza, kwa kuwa hawafahamiani kabisa, kila mmoja hujaribu kujiheshimu kwa muda, na kweli kwa muda huo huheshimika mbele ya wasiomjua.
Lakini kwa kadiri wahusika wanapokaa pamoja kwa mudaa mrefu zaidi, kila mmoja huanza kujivua “heshima bandia” aliyokuwa amejivika kwa muda na kuonesha baadhi ya tabia zake.
Hali hii hutokea katika mijumuiko mbali mbali inayokutanisha watu wageni kwa ajili ya matukio au shughuli za kijumuiya. Maeneo kama mashuleni, kambini, makazini, makazi mapya na katika majengo ya mikutano na ibada na kadhalika.
Kuanzia hapo viwango vya heshima ambavyo muhusika alikuwa amejipatia mioyoni mwa wasiomjua, tayari huanza kupoteza mvuto, tena huendelea kufifia zaidi kwa kadri muhusika anavyozidi kuonesha madhaifu yake ya kitabia.
Iko mifano mingi katika jamii ya baadhi ya watu walioupata umaarufu wa kuheshimiwa, na baada ya wahusika kuanza au kuweka hadharani vitendo visivyokubaliana na heshima stahiki, ghafla wamepoteza heshima zao!
Viashiria vya kupoteza heshima
Hivi mtu atajuaye kwamba amepoteza heshima mbele ya waliokuwa wakimheshimu? Kitu cha kwanza ni kupoteza sifa zile alizokuwa akizipata muhusika. Kama alikuwa anapongezwa kwa mambo yale ambao yamepatia heshima, sasa anaanza kupata lawama badala ya pongezi.
Kama alikuwa ana wafuasi wengi wanaomsikiliza, mara anapoteza wafuasi kwa sababu kile walichokuwa wanakifuata hakipo tena, au kimechuja kwa sababu watu wamepoteza imani naye.
Kama muhusika alikuwa akitoa huduma bora kwa watu wengi ambao walikuwa wanapenda huduma zake; baada ya muhusika kuchakachua viwango vya ubora wa huduma zake, hupoteza wateja wake kwa kuwa huduma hizo hazikubaliki wal kuaminika kama hapo awali.
Naomba nitoe angalizo hapa mapema. Si kila mwenye wafuasi wengi, au wateja wengi anafuatwa kwa kuwa anafanya mambo ya heshima. Ziko huduma zisizo na heshima, na hivyo hata wafuasi au wateja nao pia; hata kama ni wengi sana huenda ama hawajali mambo ya heshima ya mtu au wenyewe binafsi pia hawana heshima.
Kwa hiyo “wingi” wa wafuasi au wateja sio kigezo pekee cha kuthibitisha heshima ya mtu. Heshima ya mtu hutambulika kwa tabia na mwenendo wa aina ya huduma anazozitoa sambamba na aina ya wafuasi au wateja wake.
Madhara ya kupoteza heshima
1.     Kuvunja imani za wengine
Kama tulivyokwisha kudokeza huko nyuma ni kwamba, mtu maarufu anaposhindwa kutunza heshima yake, sio kwamba anaacha kuheshimika kama hapo awali; bali hii huleta madhara mengine kwa wale waliokuwa wakimheshimu. Madhara yenyewe ni wafuasi au wateja kupoteza imani na mtu mwenyewe.

 Kupoteza imani na mtu hakuishii kumpuuza muhusika peke yake, bali waathirika hupoteza imani na wengine wenye kutoa huduma zinazofanana na yule aliyechakachua maadili ya huduma husika. Wengi hujenga mtazamo hasi dhidi ya wengine ambao hata kama wao bado wanajiheshimu; nao pia huanza kushukiwa vibaya kwamba huenda hata wao wanafanana na huyo; kwa tafsiri ya mithali isemayo kwamba “Samaki mmoja akioza, wote wameoza”!
Kimsingi, kipengele hiki ndicho kinachobeba uzito wa makala na mada hii. Nasema hivi kwa sababu nimeshuhudia na wengine ni mashahidi katika hili. Hivi sasa sio siri kwamba huduma nyingi za kikanisa ziko kwenye mazingira tata na hatarishi.
Kashfa nyingi zinazowaandama wale wanaoitwa “watumishi wa Mungu” au “wakuu wa dini” au “viongozi wa taasisi binafsi za kiroho” zimechafua imani za wafuasi wengi kiasi kwamba “imani za wengi zimeathirika”! Watu wengi sio kwamba waanazidi kupoteza imani na watumishi wa huduma za kikanisa, bali wanapoteza imani na Mungu huyo anayehubiriwa na hao “watumishi bandia”!
2.     Kufilisika
Madhara mengine yatokanayo na kupoteza heshima, ni pamoja na muhusika kuishiwa na kufikia ukomo wa ubora wa huduma alizokuwa anazitoa hapo awali. Kinachosalia ni “bora huduma” badala ya “huduma bora”! Kukoma kwa ubora wa huduma pia husababisha kukoma kwa mapato yaliyokuwa yakiambata na huduma bora. Hii ndio maana ya kufilisika.
Madhara ya kufilisika ni pamoja na kushindwa kumudu gharama za uendeshaji huduma pamoja na matumizi binafsi nayo kuathirika. Katika mazingira ya jinsi hii, muhusika hulazimika ama kuuza vitu vya thamani ili kulipa bili na madeni huzidi huongezeka.
3.     Maradhi
Kupoteza heshima sio kitu kidogo na rahisi. Japokuwa hapo mwanzo muhusika anaweza kujifanya hajali sana na kujitetea kwa maneno mengi; lakini kwa ndani ya nafsi tayari anayo maumivu makali ambayo hatimaye humletea maradhi yatokanayo na maumivu ya hisia hasi. Maradhi hayo ni pamoja na “msongo wa mawazo” (Stress) au “mfadhaiko wa mawazo” (Depression)!
Magonjwa kama shinikizo la damu, kisukari, hata saratani ni baadhi ya chanzo kikuu ni mfadhaiko na msongo wa mawazo ambapo muhusika katika kujituliza hujikuta akila na kunywa vyakula ambavyo huathiri afya yake pasipo yeye kujua.
4.     Kufupisha maisha
Hapa sasa mambo yakifikia kilele cha kero ndipo muhusika huamua kufanya maamuzi magumu. Wengi hujiua kwa ama kujinyonga, kunywa sumu, au kujipiga risasi. Kwa bahati mbaya watu wengi wana tafsiri potofu kuhusu kifo. Wanadhani kufa ni kuepukana na shida na matatizo ya duniani na kupumzika milele. Kwa dhana hii wenye kujiua wanadhani wakifa watapumzika. Kumbe ndiyo wameanza awamu ya pili yenye mateso yasiyokoma milele!
Kilele cha mambo yote
ni hukumu ya milele

Katika kifungu kidogo cha 4 hapa nimedokeza kuhusu dhana potofu kuhusu kifo. Kufikiri kufa ni kupumzika. Nilidokeza kwamba kwa wengine kufa ni kuanza awamu ya pili yenye mateso yasiyokoma. Pengine hapa niweke bayana suala hili ili kuweka waziwazi ukweli wa mambo.
Yesu Kristo alitoa mfano wa watu wawili walioishi duniani na kila mmoja wakati wa uhai wake aliishi aina fulani ya maisha ambayo yalikuwa na mwonekano tofauti katika jamii. Watu hao mmoja alikuwa tajiri na wa pili alikuwa maskini na mwenye maradhi ya ngozi. Tajiri aliishi maisha ya anasa na udhalimu wakati maskini aliishi maisha ya uchaji Mungu. Yesu alisimulia kwamba wote walikufa. Kisha Yesu akasema kila mmoja alikwenda mahali maalum kulingana na aina ya maisha aliyoishi duniani. Tajiri alikwenda kuzimu mahali penye mateso makali kupindukia. Yule maskini kwa kuwa alikuwa mchaji alikwenda mahali paitwapo “kifuani pa Ibrahimu”.
Kisa kinasimulia kwamba Yule Tajiri kule kuzimu aliweza kuwaona Ibrahimu na yule maskini Razaro na kuomba Razaro amletee angalau tone la maji kwani alikuwa akiunguua vibaya sana. Ibrahimu alimjibu kama ifuatavyo: “Mwanangu kumbuka ya kwamba wewe uliyapokea mambo mema yako katika maisha yako, na Lazaro vivyo hivyo alipata mabaya; na sasa yeye upo hapa anafarijiwa, na wewe unaumizwa…..” Unaweza kusoma kisa kizima katika Luka 16:19-31)
Nilichotaka kusisitiza hapa ni kwamba, si kila mfu afaye huenda kupumzika. Inategemea mfu husika aliishi aina gani ya maisha machoni pa Mungu. Pili, mahali aendako mtu baada ya kufa hutegemeana na uchaguzi wa maisha aliyoishi duniani.
Mfano wa tajiri alioutoa Yesu hakuma akilaani utajiri wa Yule tajiri, bali alikuwa akionesha “matumizi mabaya ya utajiri” ambayo ndiyo yalisababisha aende kuzimu kwenye maumivu makali. Matumizi ya tajiri yalikuwa ni kuvaa na kula kwa anasa duniani.
Alikataa kutumiia mali zake kuwasaidia maskini, hata wale walioletwa mbele zake aliwapuuza kwa kuwatupia makombo akiwemo Lazaro. Ndiyo maana alipokufa ilibidi apokee laana nyingi kuzima badala ya Baraka:“Mwenye kuwagawia masikini hatahitaji kitu, bali afichaye macho yake atakuwa na laana nyingi.” (Mith.28:27);
Hitimisho
Nataka kumaliza kwa kauli ya mada hii ya kwamba, “ukiheshimiwa heshimika”! Tumesoma kwamba juhudi katika kutafuta mali na umaarufu si dhambi. Lakini baada ya kuvipata unavitumiaje, na wewe mwenyewe tabia yako inasomekaje mbele za wengine katika jamii. Tumepitia uchambuzi wa baadhi ya wengi wenye kufanikiwa duniani wakaheshimiwa kwa mafaniko, na kisha hushindwa kutunza heshima zile walizozipata; hatimaye kujikuta wanapoteza heshima hizo. Tulijifunza kuhusu tatizo la kujikinai baada ya kufanikiwa. Naweza kusema kwamba kwa walio wengi changamoto sio kufanikiwa, bali ni jinsi ya kuyatunza mafanikio yenyewe.
Binadamu hujisahau upesi hata kusahau kule alikotoka. Haya basi hilo linaweza kuzungumzika. La kushangaza zaidi ni binadamu kutokujali kule aondako! Na miye napenda kukumbusha tena, na kwa wengine, hii yaweza kuwa ni onyo la mwisho kwa wahusika. Mungu amesema waziwazi katika neno lake kwamba:
“Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu Yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.” (Mdo.17:30-31)
“Kwa maana imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri ya alivyotenda, kwamba ni mema au mabaya.” (2 Kor.5:10)
“hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.” (Mhu.12:13-14)
“Ukeheshimiwa heshimika”
mwisho

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni