Kwenye toleo lililopita tulipitia vipengele vinavyohusu
magonjwa kwa kujibu swali kwamba “Ikiwa Yesu alibeba magonjwa yetu yote
kwanini bado tunaugua?” Majibu tuliyopitia yalikuwa ni pamoja na: Dhambi kuendelea kupewa nafasi ya kutawala; Mtazamo
kuhusu nafasi ya magonjwa katika miili yetu; na Mashambulizi ya Ibilisi ya kupima imani yetu.
Leo tuendelee kujikumbusha kuhusu nukuu za maandiko yanayotangaza kazi ya ukombozi wa Yesu msalabani; na kisha tutakwenda kujibu maswali magumu ya umaskini wa kipato kuendelea kutawala ulimwengu wakati Yesu alifanyika maskini ili sisi tuwe matajiri kwa umaskini wake:
Leo tuendelee kujikumbusha kuhusu nukuu za maandiko yanayotangaza kazi ya ukombozi wa Yesu msalabani; na kisha tutakwenda kujibu maswali magumu ya umaskini wa kipato kuendelea kutawala ulimwengu wakati Yesu alifanyika maskini ili sisi tuwe matajiri kwa umaskini wake:
Marejeo kuhusu Kazi ya Ukombozi wa Yesu
Msalabani
Marejeo kuhusu Kazi ya ukombozi
iliyofanywa na Yesu msalabani ni muhimu sana katika mfululizo wa makala haya
kwa sababu zifuatazo: Moja, si kila msomaji anayesoma makala haya alianza nasi
tangu mwanzo wa makala yenyewe. Kwa hiyo anahitaji kujua kiini cha makala na
matarajio yake ni nini. Pili, tunaporejea kusoma maandiko kuhusu ya ukombozi
kwenye makala haya tunajiwekea mwongozo wa kutujengea nidhamu ya kujifunza
pasipo kutoka nje ya mada.
Kwa hiyo, tunaposema “Kazi ya Ukombozi
iliyofanywa na Yesu Msalabani; kimsingi tunamaanisha mambo makuu matatu
yafuatayo: 1 Dhambi, 2. Magonjwa, 3. Umaskini wa kipato.
Kwa habari ya dhambi tunashuhudia kimaandiko pale
Paulo alipowakumbusha Wakorintho akisema: “Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi
kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika yeye.” (2.Kor.5:21)
Kwa habari ya magonjwa tunashuhudia kimaandiko
pale Mathayo alipoandika katika Injili akisema: “Hata kulipokuwa jioni,
wakamletea wengi wenye pepo; akawatoa pepo kwa neno lake, akawaponya wote
waliokuwa hawawezi, ili litimie line neno lilonenwa na nabii Isaya, akisema,
Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, na kuyachukua magonjwa yetu.” (Matt.8:16-17)
Kwa habari ya umaskini wa kipato tunashuhudia
kimaandiko pale Paulo alipowakumbusha Wakorintho akisema: “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi
alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi
mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.” (2.Kor.8:9)
Mpendwa msomaji! Kwa kuwa baadhi ya nukuu za maandiko haya
zilikwisha kuchammbuliwa katika makala za nyuma; na kwa kuwa huenda msomaji
hukupata nafasi ya kusoma yaliyokuwemo; ili kukujengea mtiririko makini napenda
kurejea kwa ufupi sehemu ya vipengele muhimu vinavyohusu falsafa ya ukomboai
katika tawi lake la umiliki:
Maono asilia ya Mungu kuhusu binadamu
Kwa wale tunaoamini kwamba
binadamu ameumbwa na Mungu kama livyoandikwa katika Biblia, tunao ushahidi wa
kimaandiko kwamba maono ya Mungu kuhusu binadamu hayakuwa na nia ya kumfanya
binadamu kuwa fukara na maisha ya fujo na ghasia duniani.
Tukisoma maandiko kuhusu maono ya
Mungu juu ya binadamu tusoma kwamba: “Mungu
akasema na tumfanye mtu kwa mfano wetu; na kwa sura yetu; wakatawale…..”
(Mw.1:26)
Andiko hili linadhihirisha bayana
kusudi la Mungu kuhusu binadamu hata kabla hajamuumba. 1. Kuumbwa kiumbe
anayeshabihiana na Mungu kwa fikra, hisia na utashi; 2. Kuumbwa kiumbe
atakayemwakilisha Mungu katika utawala wa dunia na viumbe vyote vilivyomo.
Kutokana na Maono haya Mungu
aliyatimiza kwa kuwaumba binadamu wa kwanza, Mwanamume na mwanamke, kama
ilivyoandikwa: “Mungu akaumba mtu kwa
mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu
akawabarikia, Mungu akawaambia, zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na
kuitiisha; mkatawale…..” (Mw.1:27-28)
Kutokana na ushahidi wa kimaandiko
tuliyosoma hapa juu, tunathibitisha kwamba binadamu wa kwanza waliumbwa katika
hali ya utukufu wa Mungu, na wakamilikishwa kuitawala nchi na viumbe vyote
vilivyomo. Kwa maelezo mengine ni kwamba, haki na mamlaka ya kumiliki ni
ya kimaumbile. Hisia ya kumiliki ni sehemu ya maumbile ya kila binadamu.
Pasipo kujali binadamu yuko katika
mazingira ya aina gani hisia ya kumiliki imo ndani yake. Maswali mengi
yanayojitokeza ni kama huu ndio ukweli tena wa kimaumbile kwa kila binadamu,
kwanini basi hivi sasa kuna matabaka ya maskini na matajiri, watumwa na mabwana,
waajiri na wajiriwa? Majibu ya maswali haya yanatupeleka kwenye sehemu ya pili
ya falisafa ya umilikishaji.
Kuvunjika kwa mahusiano na kupoteza mamlaka
Baada ya binadamu wa kwanza kuumbwa, na kumilikishwa kama
Mungu alivyowakusudia, binadamu hao hao walifanya maamuzi mabaya ambayo
yaliwagharimu matokeo mabaya. Mungu alipowamilikisha aliwapa sheria ya kutokula
matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, na akawaonya kwamba siku
watakapokiuka sheria hiyo, watavunja mahusiano na yeye, na pia watapoteza sio
mamlaka ya utwala peke yake, bali wasitisha na maisha ya umilele duniani.
Adamu na Eva walipokiuka sheria ya Mungu; ghafla wakajikuta
wamefarakana na Mungu kama livyoandikwa: “…kwa sababu wote wamefanya
dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu;..” (Rum.3:23)
Kwa bahati mbaya, uvunjwaji wa sheria ya Mungu ulifanywa na
binadamu wa kwanza wale wale ambao ndio walitakiwa kubaki mfano wa vizazi vya
binadamu vinavyofuatia. Biblia imeandikwa kwamba:“Kwa hiyo, kama kwa mtu
mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi
hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Rum.5:12)
Kutokana na maandiko tunaona kwamba kwa kosa la binadamu
kuliathiri vizazi vyote vya binadamu waliofuata baada yao. Na athari
hazikuishia katika kupoteza utukufu wa Mungu, bali ulisababisha kunywang’anywa
ile mamlaka ya utawala. Lakini Mungu atukuzwe kwa sababu hakuridhika na athari
zilizomsibu binadamu bali aliandaa mpango maalum wa kumkomboa na kumrejesha
katika asili yake ya kwanza. Mpango huu tutaupitia katika makala yajayo.
Mpango wa pili wa Mungu ukombozi wa
binadamu
Baada ya binadamu wa kwanza kupoteza haki, mamlaka na fursa
za kumiliki, na kusababisha athari mbaya za mapigo ya magonjwa na umaskini wa
kipato; Mungu aliamua kuonesha upendo wake kwa binadamu kwa kumtuma Mwanawe
Pekee ulimwenguni kama tunavyosoma: “Kwa maana jinsi hii, Mungu aliupenda
ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe
pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na zima wa milele.” (Yh.3:16)
Ujio wa
Yesu Kristo duniani ulibeba misheni yenye mambo mawili muhimu ambayo binadamu
aliyapoteza ambayo ni: i) Kurejesha mahusiano yaliyovunjika
kati ya binadamu na Mungu ii) Kurejesha mamlaka aliyonyanganywa binadamu na
Ibilisi.
Kwa habari ya kurejesha mahusiano yaliyovunjika kati ya
binadamu na Mungu, Yesu Kristo alikuja akiwa kufanyika dhabihu ya dhambi
iliyomtenga binadamu na Mungu kama ilivyoanidkwa:“Siku ya pili yake
akamwoma Yesu anakuja kwake, akasema, Tazama Mwakandoo
wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu!” (Yh.1:29)
Kupitia
mateso na kifo cha Yesu Msalabani, Yesu aliupatanisha ulimwengu na Mungu kwa
yeye kulipa fidia ya adhabau ya dhambi, tena ya kosa la binadamu wa kwanza.
Lakini kwa Yesu kushuka kuzimu na kufufuka katika wafu kulisababisha kurejeshwa
mamlaka zote zilizoporwa na Ibilisi pamoja na haki ya kumiliki.
Mtume
Yohana aliyekuwa mwanafunzi aliyependwa sana na Yesu, anatusimulia katika
Injili aliyoiandikwa akisema kwamba, ujio wa Yesu Kristo ulilenga kurejesha
mamlaka ya kifalme kwa wote watakaomwamini Yesu Kristo:“Bali wote
waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio
jina lake.” (Yh.1:11)
Tendo
la mtu kufanyika mtoto wa Mungu limebeba ahadi na mamlaka ya kumiliki mali za
mfalme, ambaye ni Mungu Baba, kwa kupitia Mwanawe Pekee. Huwezi kufanyika mtoto
wa mfalme ukaendelea kuishi maisha ya ufukara, labda kama unafanya igizo!
Majibu ya maswali nyeti kuhusu nadharia
ya kumiliki
Ninafahamu kwamba yako maswali sugu tena ya miaka mingi
ambayo huulizwa na kila mwenye mashaka na nadharia ya kumiliki. Maswali hayo ni
kama haya yafuatayo: i) Hivi huu Ukombozi
wa Yesu Kristo kwa binadamu ni maisha ya sasa au siku ya kiyama? ii) Kwanini
wengi wanaodai kumfuata Yesu Kristo maisha yao ni yale yale ya mateso na
umaskini wa kipato? Iii) Je Yesu mwenyewe si alishasema kuwa ulimwenguni tunayo
dhiki, na mitume wake nao wakathibitisha kwamba tunaingia mbinguni kwa
njia ya dhiki nyingi?
Majibu ya maswali haya ni muhimu
sana kwa kila asomaye makala haya, na bila shaka atapata fursa ya kuzipima
nadharia zilizopo na majibu yangu:
1. Majibu ya ukombozi wa Yesu ni maisha ya
sasa au siku ya kiyama?
Ukombozi wa Yesu Kristo kwa binadamu ni
maisha ya sasa na kilele chake ni kunyakuliwa kwa kanisa duniani. Ukifuatilia
kwa makini katika Injili zote kuhusu maisha ya Yesu Kristo duniani, utakuta
alihubiri Injili ya ufalme iliyoambatana na udhihisho wa mamlaka ya kifalme
katika kutatua matatizo sugu matatu: kusamehe dhambi, kuponya ulemavu na
magonjwa yote; na kushughulikia mahitaji ya chakula yalipojitokeza.
Aidha, kanisa la kwanza lililoanzishwa
na mitume jijini Yerusalemu nalo lilidhihirisha maisha ya kifalme kwa
kuhakikisha watu wanatubu dhambi na kuzaliwa mara ya pili, kuponywa magonjwa
yote, na kila aliyejiunga na kanisa hilo aliacchana na umaskini wa kipato. Kwa
hiyo maisha ya ukombozi wa Yesu Kristo yanaanzia hapaa hapa duniani kama
yalivyodhihirishwa na Yesu Kristo, mitume wake na wakristo wa kanisa la kwanza!
Hata hivyo, bado mchakato wa kumiliki
unaendelea na utafikia kilele chake wakati Yesu Kristo atakapolichukua kanisa
lake na kwenda kukaa nalo pale mahali aliposema anakwenda kuliandalia makao.
Kwa kusema haya, sipuuzii uhalisia wa
mambo jinsi yanavyoonekana kwa macho hapa duniani kwa hivi sasa. Uhaalisia
unaonesha jinsi ambavyo maisha ya wengi waitwao wachaji Mungu, wafuasi waamini
wa Yesu ni duni na kujaa changamoto nyingi za kiuchumi. Mimi pia nimepitia
maisha haya haya tangu mwanzoni mwa uchanga wa imani yangu katika Kristo na
mapokeo niliyofundishwa hapo awali.
Naomba nijibu sio kama majivuno bali
kwa unyenyekevu mkubwa kwamba, changamoto zote zinazoonekana hivi sasa,
hazitokani na wala sio sehemu ya Injili ya Yesu Kristo na Mitume wake. Haya ni
matunda ya ukengeufu wa karne nyingi huko nyuma ambao ulizalisha “Ukristo
bandia” katika ulimwengu huu!
Nadharia ya kwamba, maisha ya dhambi na
umaskini ndio dhiki za mkristo duniani mpaka Yesu atakaporudi mara ya pili; ni
matokeo ya ukengeufu ule ambayo Yesu Kristo mwenyewe aliutabiri kuwa utakuja na
kuwakumba walio wengi! Kumbukeni mfano wa ngano na magugu ambao Yesu aliwaambia
waanfunzi wake na tafsiri aliyoitoa.
Ukristo bandia umeshika nafasi kubwa
ulimwenguni kwa kuwaaminisha watu kuishi katika dhambi kisha kuungama na
kuendelea maisha ya dhambi kanisani; badala ya kuzaliwa mara ya pili na kupokea
uwezo wa kushinda dhambi (wanaona ni fahari kuitwa wenyedhambi)
Hata kwa
wale wanaopokea neema ya kuujua Ukristo wa kweli, na kuzaliwa mara ya pili, kwa
sababu ya mapokeo ya ukristo bandia, bado huendelea kuaminishwa kwamba, maisha
ya umaskini wa kipato ni njia mojawapo ya utakatifu, na kwamba kumiliki
uchumi ni tamaa za kiulimwengu. Kwa imani hii, huendelea kuishi maisha
duni, ambayo matokeo yake walio wengi huiacha imani na kurudi duniani.
Lakini tukumbuke kwamba KANISA LA
KWANZA kwa muda wa miaka 40 mfululizo, likiwa na zaidi ya washirika 30,000 lilidhihirisha
maisha ya ukombozi wa Kristo duniani; dhambi ilikemewa, wagonjwa wote
waliponywa, na hapakuwepo miongoni mwao hata mmoja aliyekuwa maskini wa kipato!
2. Majibu kuhusu dhiki iliyotajwa na Yesu na
mitume wake
Neno hili “dhiki” limekuwa
likitafsiriwa kinyume ili kuhalalisha maisha ya mikandamizo ya kipepo, nagonjwa
na umaskini wa kipato kwa wachaji Mungu kanisani. Yametumika kama faraja lakini
nyuma yake ni mbinu za adui za kufanya wahusika kuchukuliana na maisha haya kwa
kudhani ni mapenzi ya Mungu wawe hivyo haoa duniani!
Kwa kifupi Maneno ya Matoleo ya Biblia
za Kiingereza yaliyotumika kutafsiri neno hili “dhiki” ni “hard times”
“persecutions” na “tribulations”! Tafsiri ya maneno haya ni “Nyakati ngumu”,
“mateso” na “mateso makali” au adha! Hapa hatusomi habari za dhiki kuitwa
“magonjwa” wala “umaskini uliokithiri”!
Baadhi ya maandiko ambayo yametumiwa
sana ni kauli ya Yesu Kristo aliwapowambia kwmaba: “..Hayo nimewaambieni mpate kuwa
na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi
nimeushinda ulimwengu.” (YH.16:33)
Maana ya neno “dhiki” lililotajwa hapa
ni upinzani mkali dhidi ya imani katika Kristo ;upinzani wenye kuambatana na
vitisho, na mateso ya mapigo ya viboko, na vifungo vya gerezani. Hii ndiyo dhiki aliyomaanisha
Yesu. Isitoshe, Yesu aliwoanya pia wanafunzi wake kwamba sio kwamba watateswa
kwa sababu ya imani yao kwake, bali hata kuuawa pia: “watawatenga na masinagogi; naam,
saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada.”
(Yh.13:2)
Baada ya Yesu kupaa, na mitume wake
kuchukua nafasi ya kuhubiri Injili ambayo ilikuwa imepigwa marufuku na wakuu wa
dini na dola, ndipo yalipotimia maneno ya Yesu Kristo ya kupatwa na “dhiki
nyingi” ambazo zimetajwa na Luka alipoandika: “Wakifanya imara roho za
wanafunzi na kuwaonya wakae katika imani, na ya kwamba imetupasa kuingia katika
ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi.” (Mdo.14:22)
Majumuisho ya
majibu ya maswali
Kama nilivyokwisha kuanisha hapa juu, nadharia
ya kumilikisha ni urithi wa Agano Jipya kwa wote wanaomjia Yesu Kristo.
Ukombozi wa Yesu Kristo unajumuisha msamaha wa dhambi, unaosababisha kufutwa
kwa adhabu ya maradhi na umaskini wa kipato. Jamii ya waaminio imeahidiwa
kuishi maisha ya kifalme duniani na kilele chake ni mbinguni Yesu
atakapolichukua kanisa lake. Dhiki inayotajwa duniani sio umaskini
wa kipato bali chuki na upinzani dhidi ya imani
unaoambatana na vitisho na mateso ya kimwili pamoja na kuuawa inapobidi.
Ni kweli kabisa kwamba Mkristo halisi,
kuna nyakati maalum ambapo atapitia kwenye mapito magumu ya kiuchumi; ikiwa ni
mashambulizi ya ibilisi ambaye anajua uchumi ukiwa mikononi mwa Mkristo
utatumika kubomoa ufalme wake. Hata hivyo, pamoja na ukweli kwamba Mkristo
hupitia mapito magumu ya kiuchumi; bado mapito hayo nayo ni ya mpito pia; na
wala sio kuwa huu ndio mfumo wa maisha ya Mkristo halisi duniani!
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni