YESU NI JIBU

Jumamosi, 17 Mei 2014

FALSAFA YA UKOMBOZI KWA MUJIBU WA BIBLIA SEHEMU YA TATU



Ni matumaini yangu msomaji wa blog hii ya amaninafuraha kuwa unaendelea kupata mafundisho sahihi kutoka kwa mtumishi wa MUNGU askofu mkuu wa WAPO Mission International juu ya falsafa mbalimbali kwa mujibu wa biblia sasa kazi kwako kuamini na kutendea kazi na ni imani yangu kuwa utafunguliwa na kuwa huru katika maisha yako ya kila siku.


Zaidi ya yote utaanza kumiliki kwa mujibu wa biblia sasa endelea kuungana na mtumishi wa MUNGU
Kwa siku zilizopita, tulijifunza kuhusu kazi aliyofanya Yesu Kristo msalabani kwa kuivinja nguvu ya dhambi isipate kutawala katika miili yetu; ili sisi tuishi maisha ya ushindi dhidi ya dhambi katika ulimwengu huu wa sasa. Aidha, tulijifunza pia kwamba dhambi kuendelea kutawala katika miili ya waamini wa leo; siyo kwa sababu bado ina nguvu kama kabla Yesu hajasulubiwa msalabani; bali ni kutokana na “kutokubadili mtazamo wetu kuhusu nafasi ya dhambi ulimwenguni”, na kwamba kwa njia hii na kwa ridhaa yetu tunaipa dhambi nguvu ya kuendelea kutawala! Mwisho tulikomea kwamba toba na ubatizo ni kielelezo cha imani kinachoifanya kazi ya Kristo iwe halisi katika maisha ya kila anayemwamini. Leo tunaingia kwenye jambo la pili ambalo Kristo alilishughulikia msalabani ambalo ni magonjwa:
Ikiwa Yesu alibeba magonjwa
yetu yote kwanini bado tunaugua?

Kama ambavyo kazi ya Yesu Kristo msalabani ilivyovunja nguvu ya dhambi; hali kadhalika na magonjwa yote nayo yalishughulikiwa kwa wakati mmoja, na kwa mara moja kama ilivyotabiriwa na mtunga Zaburi alipotabiri akisema:
 “Akusamehe maovu yako yote, akuponya magonjwa yako yote, aukomboa uhai wako na kaburi, akutia taji ya fadhili na rehema, ushibisha mema uzee wako, ujana wako ukarejezwa kama tai;..” (Zab.103:3-5)
Maandiko haya yanatabiri waziwazi kuhusu ujio wa Yesu Kristo na kazi ambayo angeifanya kwa ajili ya dhambi pamoja na magonjwa. Anaweka bayana kwamba, dhambi itashughulikiwa 100% na magonjwa nayo yatashughulikiwa 100%!
Hata kabla Yesu hajasulubiwa msalabani alionesha mamlaka kamili ya kusamehe dhambi na kuponya magonjwa yote, pamoja na kufukuza pepo wachafu ambao ndio mawakala wa magonjwa yote:
“Hata kulipokuwa jioni, wakamletea wengi wenye pepo; akawatoa pepo kwa Neno lake, akawaponya wote waliokuwa hawawezi, ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu.” (MT. 8:16, 17)
Maana kamili ya Yesu kubeba magonjwa yetu, haina maana kwamba aliugua magonjwa yenyewe alipokuwa juu ya msalaba. Maana yake hasa ni kwamba Yesu alipokuwa msalabani, mwili wake ulibeba maumivu na mateso yatokanayo na aina zote za magonjwa ya binadamu. Aliuhisi uchungu na maumivu ya aina zote ya binadamu wote, wa vizazi vyote.
Kwa njia hii, nguvu za magonjwa ziliharibiwa juu ya mwili wa Yesu, ili kwamba, magonjwa yote yasitawale tena katika miili ya wote watakaoikubali na kuitambua kazi aliyoifanya Yesu msalabani.Yesu alipofufuka katika wafu, alifufuka na mwili mpya wa utukufu ambao, huo pia ni ahadi kwa kila anayemwamini Yesu ataupokea baada ya maisha ya duniani kufikia ukomo.
Mpango wa ukombozi wa Kristo, ni pamoja na kuishi maisha yenye afya bora, pasipo magonjwa kabisa. Huu ni ukweli wa kibiblia tena kwa Agano Jipya. Maisha huru mbali na magonjwa. Ukweli huu unaweza kuwa mgumu kuuamini kwa binadamu wa kizazi hiki, lakini Neno la Mungu lenyewe halibadiliki vizazi vyote.
Sasa turudi kwenye swali letu la msingi. Ikiwa kweli Yesu alisulubiwa na kwa kupigwa kwake ili kila amwaminiye apate fursa ya kuwa na afya njema pasipo maradhi; mbona bado magonjwa yanawaandama wale waitwao wafuasi wa Kristo? Nilisema kwamba kuna sababu. Kila ugonjwa unapoingia katika mwili wa binadamu una sababu. Kumbuka kwamba ugonjwa siyo sehemu ya maumbile ya binadamu. Ndiyo maana unapoingia katika mwili wa binadamu unasababisha maumivu, mateso, kero na usumbufu wa kiafya. Lakini kila uingiapo ugonjwa kuna sababu. Na katika kujibu swali la msingi nitazitaja baadhi ya sababu hizo kama ifuatavyo:


1.  Bado dhambi imepewa nafasi ya kutawala
Sehemu ya makala iliyopita nilichambua sababu za dhambi kuendelea kutawala hapa ulimwenguni, hususan kati ya jamii ya wale wanaomwamini Yesu; kwamba ni “mtazamo ambao haujabadilika kuhusu nafasi ya dhambi ulimwenguni.” Nilisema kwamba kama mtu hajabadili mtazamo wake kuhusu nafasi ya dhambi ulimwenguni, na kwamba bado anaamini bado dhambi ingali na nguvu zake katika maisha ya mwamini mpaka sasa, basi dhambi itaendelela kutawala kana kwamba Yesu Kristo hajawahi kuja duniani na kusulubiwa msalabani.
Sasa tukisimamia katika ukweli huu, tunapata jibu la leo la  ni kwanini bado magonjwa yanaendelea kutawala ulimwenguni. Kutokubadili mtazamo kuhusu dhambi ndio mlango wa magonjwa nayo kuendelea kutawala pia? Haviachani kabisa. Kama alivyosema: akusamehe maovu yako yote na akuponya magonjwa yako yote; hali kadhalika, kama mtazamo wa kuondolewa dhambi bado una mushkeli, magonjwa nayo yanafunguliwa mlango wa kuwepo kwa sababu; kila mahali dhambi ilipo na magonjwa nayo hapo ndio mahali pake! Kwa maelezo mengine, dhambi ni kivutio cha magonjwa. Labda nimnukuu Bwana Yesu mwenyewe katika suala hili:
“Baada ya hayo Yesu akamkuta ndani ya hekalu, akamwambia, angalia, umekuwa mzima; usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lililo baya zaidi.” (Yh.5:14)
Hii ni mara ya pili kwa Yesu kutamka kauli ya katazo la aliyesamehewa dhambi asitende dhambi tena. Mara ya kwanza alimwammbia Yule mwanamke aliyekamatwa kwenye uzinzi akaletwa ili apigwe mawe na iliposhindikana akaachwa huru na Yesu akamtamkia akisema: “usitende dhambi tena”. Lakini katika maandiko haya Yesu anaongeza kusema madhara yatokanayo na kuponywa magonjwa na kurudi katika maisha ya dhambi hatimaye husababisha magonjwa makubwa zaidi kuliko yale yaliyokuwepo kabla. “usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lililo baya zaidi….”
2.  Mtazamo kuhusu nafasi ya magonjwa katika miili yetu
 Sababu ya pili ni “kutokubadili mtazamo kuhusu nafasi ya magonjwa” katika ulimwengu wa sasa na katika maisha ya mwamini. Hapa ninachomaanisha ni kwamba, si kila ugonjwa unaompata mwamini ni kwa sababu ametenda dhambi ya aina fulani. La hasha.
Lakini kama mwamini kimtazamo bado anafikiri na kusadiki kwamba “kuugua ni sehemu ya maisha yake” ;na “kwa sababu bado anao mwili wa mauti” na kwa hiyo “kuugua ni lazima” kwake; basi kwa mtazamo huo peke yake unatosha kuyaruhusu magonjwa kufanya makao katika mwili wake!  Hii ndiyo kweli tupu hata kama inauma na kuudhi! Narudia tena, kama ilivyo kwenye “kutokubadili mtazamo kuhusu dhambi” kunaifanya dhambi iendele kutawala; ndivyo ilivyo hata kwa magonjwa pia!
Narejea kusema tena ya kwamba, japokuwa magonjwa mengine huwapata waamini kwa sababu ya kuishi katika dhambi kimtazamo na kitabia; sio kila ugonjwa unatokana na dhambi. Lakini kuamini kwamba ni wajibu kuugua ni mlango kamili wa kuita magonjwa yaje mwilini kwa sababu yamekaribishwa na mhusika kwa hiari yake mwenyewe.
3. Mashambulizi ya Ibilisi  ya kupima imani yetu
Sasa tunakuja kwenye sababu ya tatu. Tumekwisha kupitia sababu mbili za mwanzo ambazo, kimsingi, chanzo chake ni kutokana na mhusika binafsi.. Lakini sababu ya tatu hii ni mashambulizi kutoka kwa Shetani na malaika zake. Tukumbuke kwamba, kama vile ambavyo bado Shetani ameruhusiwa kuwajaribu/kuwashawishi waamini kwa habari ya dhambi; hali kadhalika Shetani huyo huyo hutumia vitisho vya magonjwa ili kutikisa imani za waamini.
Mashambulizi haya huwapata waamini kwa muda fulani ili kujaribu ufahamu walio nao kuhusu “kazi iliyofanywa na Yesu msalabani ya kubeba magonjwa yetu yote” na kwamba kwa muda wote ambao uhusiano wetu na Mungu ni safi; Shetani hana mamlaka ya “kupandikiza magonjwa” yake katika miili yetu.
Kimsingi, mashambulizi haya yanapompata mwamini, kazi yake ni kutumia mamlaka ya Jina la Yesu kukemea, kufukuza au kuamuru magonjwa hayo yasifanye makazi katika mwili wake. Narejea tena hapa kwamba hili ni suala la “mtazamo wa mwamini” kukumbuka kwamba ugonjwa hautakiwi kufanya makazi katika mwili wake kwa mujibu wa kazi iliyofanywa na Yesu Kristo msalabani!
Na hapa ndipo penye changamoto kweli kweli. Wengine wanatafsiri kwamba, pamoja na mashambulizi ya Shetani, bado mtu wa Mungu na yule aliyejitoa kumtumikia Mungu kwa uaminifu; ati hapaswi kuugua kwa namna yoyote. Pengine wenye mtazamo huu wamepitiliza kiasi.
Nasema wamepitiliza kiasi kwa sababu tunayo maandiko yanayoweka waziwazi baadhi ya watumishi wa Mungu walioshambuliwa na Shetani kwa magonjwa, na wengine wakanusurika hata kufa. Lakini kwa maombi na rehema za Mungu wakapokea uponyaji na kurejea katika afya zao tena. Baadhi yao ni hawa wafuatao:
“Erasto alikaa Korintho. Trofimo nalimwacha huko Mileto, hawezi.” (2 Tim.4:20)
Huyu Erasto alikuwa mwamini na mtumishi wa Injili pamoja na mtume Paulo. Wakiwa katika msafara wa Injili akashambuliwa na ugonjwa na akalazimika kulazwa na kuachwa na wenzake. Haya ushahidi wa maandiko mengine ni haya hapa chini:
“Lakini naliona imenilazimu kumtuma kwenu Epafrodito, ndugu yangu, mtendakazi pamoja name; tena ni mtume wenu na mhudumu wa mahitaji yangu. Kwa kuwa alikuwa na shauku kwenu ninyi nyote, akahuzunika sana, kwa sababu mlisikia ya kwamba alikuwa hawezi. Kwa maana alikuwa hawezi kweli kweli, karibu na kufa; lakini Mungu alimhurumia; wala si yeye peke yake, ila na mimi pia; nisiwe na huzuni juu ya huzuni.” (Flp 2:25-27)
Bila shaka kwa maandiko haya hapa tumeuthibitisha ukweli wa mashambulizi ya magonjwa kutoka kwa Shetani. Kimsingi Paulo mwenywe ameeleza waziwazi kwamba mara kadhaa walitaka kwenda mahali fulani lakini Shetani akawazuia:
“Kwa hiyo tulitaka kuja kwenu, naam, mimi Paulo, mara ya kwanza, na mara ya pili, na Shetani akatuzuia.” (1 Thes.2:18)
Kwa maandiko haya, tushuhudia kwamba Shetani amekuwa mpinzani wa Mungu na watumishi wake; na amekuwa akiweka vipingamizi vya kuzuia huduma za Injili zisiwafikie wengine wamjie Kristo.
Bila shaka msomaji unaweza kuchanganyikiwa ukifikiri kwamba, kama Shetani anaweza kutupa magonjwa kwa watumishi wa Mungu wakaugua mpaka kunusurika kufa; je hii sio kudhoofisha kazi ya Yesu iliyofanyika msalabani? Kwa mtazamo wa haraka inaweza kutafsiriwa hivyo. Lakini tukitafakari kwa kina tunaweza kuona kwamba, kushambuliwa na shetani kwa magonjwa ni tofauti na mwenye aliyeshambuliwa kuyaruhusu magonjwa hayo kufanya makao ya kudumu katika mwili wake.
Mashambulizi ya Shetani kwa magonjwa huwa ni ya kitambo maalum; na kila akipingwa na kukemewa kwa mamlaka ya Kristo pasipo kukoma lazima shetani atakimbia na magonjwa yake!! Pili, Mungu alijua kwamba shetani ataleta mashambulizi kwa watumishi wake, na ndiyo maana akamtuma Roho Mtakatifu na karama za kuponya magonjwa ili kumpinga shetani na magonjwa yake. Ndio maana hao tuliosoma katika maandiko ya kuwa walishambuliwa na magonjwa tunaona walipambana kwa maombi mpaka wakapokea uponyaji.

 
  

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni