YESU NI JIBU

Jumatatu, 5 Mei 2014

FALSAFA YA UKOMBOZI KWA MUJIBU WA BIBLIA



Falsafa ya ukombozi kwa mujibu wa Biblia-2
UNGANA NA ASKOFU GAMANYWA KUJIFUNZA FALSAFA YA UKOMBOZI KWA MUJIBU WA BIBLIA.

Mapitio kuhusu mambo makuu 3 ya UKombozi wa Kristo msalabani; Maana na sababu ya Yesu kufanyika dhambi. Leo tunaendelea na mfululizo wa makala kuhusu nafasi ya dhambi katika ulimwengu wa sasa:

Muhutasari kuhusu Maana na
sababu ya Yesu kufanyika dhambi

Kwa mujibu wa maandiko ya (2 KOR.5:21;1 PET. 2:24) tuliweza kuona kuona ugumu wa Paulo alichoandika kuwa ni: “….Yesu asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu;” na jinsi ambavyo Mtume Petro aliturahisishia tafsiri akisema: “….Mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti…” Maandiko yote haya kwa pamoja yalitufundisha kwamba:
a)    Yesu alikubali kuhukumiwa adhabu kama mkosaji lakini bila kosa kibinafsi
b)    Yesu alikubali kubeba hukumu ya adhabu kwa niaba yetu
c)     Yesu alikubali “Nguvu ya dhambi” kuharibiwa juu ya mwili wake
d)    Yesu alikusudia kwamba “Nguvu ya dhambi” isiendelee “kutawala katika miili yetu”

Aidha, maandiko ya Mtume Yohana katika (Yh.8:34;Yoh.8:35; 1 Yh.3:8) yalitufundisha sababu zilizomfanya Yesu kufanyika dhambi kwa ajili yetu ambayo ni Kutukomboa kwenye utumwa wa dhambi na Kuzivunja kazi za Ibilisi ili asiwe na mamlaka juu yetu. Leo tunaingia sehemu ya pili ambayo inashughulikia maswali magumu na majibu makini kuhusu nafasi ya dhambi katika ulimmwengu wa sasa.

Kama Yesu alivunja nguvu ya dhambi
kwanini bado inaendelea kutawala ulimwengu?

Baada ya kutoa ufafanuzi kama ilivyoanishwa hapo awali; mara yanakuja maswali mazito, magumu tena mfululizo yenye kuhoji uhalisia wa maelezo yangu. Yanakuja maswali yakihoji kuwa 1. Kama kweli Yesu Kristo aliihukumu na kuiharibu dhambi hiyo isiendelee kutawala katika maisha yetu; kwanini bado dhambi inaonekana kuendelea kutawala katika ulimwengu huu?  2. Kwanini wale tuitwao kanisa la Kristo bado tunasumbuliwa na dhambi? 

Kutokana na maswali magumu yaliyotangulia kuna nadharia na dhana nyingi ambazo zimejaribu kutoa majibu ya kuhalalisha ni kwanini mado dhambi inaonekana kuendelea kutawala. Baadhi ya majibu hayo ni pamoja na:

a)    Kazi ya Yesu Msalabani bado haijakamilika kiuhalisia mpaka hapo tutakapoondolewa katika ulimwengu huu
b)    Dhambi inaendelea kutawala katika miili yetu kwa sababu bado tuna miili ya mauti na hatujavikwa miili ya utukufu

Ukiyatazama majibu haya, yanaonekana kuwa na ushawishi mkubwa sana kwa mtu Yule ambaye anatafuta kisingizio cha kuendelea kuishi katika maisha ya dhambi. Ni majibu yanayofariji na kuhalalisha kutenda dhambi kwa visingizio vya kimaumbile. Lakini ukisoma maandiko matakatifu na tafsiri zake sahihi, utagundua kwamba majibu haya yamefunika udhaifu wa kiimani; na kuibatilisha kazi ya Kristo ambayo ilimleta hapa duniani.

Naomba nianze kujibu maswali magumu kwa kutoa majibu ya makini kwa mujibu wa maandiko yasemayo katika tafsiri yake sahihi. Ninaomba kwamba, ukweli ubaki kuwa ukweli hata kama ni mgumu kuutekeleza lakini usipindwe ili kukidhi udhaifu wetu. Jibu langu la kwanza ambalo sitaki kumung’unya maneno ni hili.

a)    Kazi ya Yesu ya kusulubishwa na kufa msalabani kwa ajili ya dhambi zetu; ililenga “kuivunja nguvu ya dhambi isipate kutawala” katika “miili yetu ya sasa ya mauti” na sio katika ulimwengu ujao tutakapovikwa “Miili ya utukufu”!

b)    Tangu dhambi ilipohukumiwa juu ya mwili wa Yesu, haina nguvu zake za asili kama ilivyokuwa kabla ya Yesu Kristo kusulubishwa juu ya Msalaba.

c)     Swali kwamba ni kwanini bado dhambi inaonekana kuendelea kutawala ulimwenguni, jibu lake ni kwamba; “bado wengi wetu hatujabadili mtazamo wetu kuhusu nafasi ya dhambi katika ulimwengu wa sasa”! Nasema tatizo ni “mtazamo wetu” na sio kwamba bado dhambi ina nguvu ile ile ya kutawala miili yetu!

Narudia tena. Kwa kuwa wengi wetu bado hatujabadili mtazamo wetu kuhusu nafasi ya dhambi katika ulimwengu wa sasa; na kwa sababu bado tunaamini kwamba dhambi bado ina nguvu ile ile kama kabla ya Yesu kusulubiwa msalabani; basi kwa sababu hiyooooo ya kimtazamoooo ndio mlango “unaoihuisha dhambi” au “kuiruhusu dhambi”  au ”kuipa nguvu dhambi” izidi kuendelea “kutawala katika miiili yetu”!

Maandiko yasemavyo na tafsiri yake
kuhusu nafasii ya dhambi ulimwenguni

Kimaandiko katika Agano Jipya, na ushahidi wa maisha ya mitume na Wakristo wa karne ya kwanza; Dhambi yenyewe katika uhalisia wake haina nguvu kabisa. Lakini kwa mtazamo wetu, na hiari hiari zetu binafsi; tumeendelea kuipa nafasi dhambi kuwa na nguvu. Nasema tena, kutokana na mtazamo wako, au kwa itikadi yako vimeipa dhambi ruksa iendelea kutawala katika maisha yako.

Baada ya kutoa majibu ya msingi, sasa nataka kuyathibitisha majibu yangu kwa maandiko matakatifu ya Mitume wetu jinsi ambavyo katika kizazi chao waliweza kuishi maisha ya udhidi dhi ya dhambi katika  ulimwengu wa sasa na kwenye miili yetu hii ya mauti. Tafadhali soma kwa makini vifungu vya maandiko yafuatayo:

 “Tuseme nini basi, tudumu katika dhambi ili neema izidi kuwa nyingi? Hasha, sisi tuliofia dhambi tutaishije tena katika dhambi? Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake? Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende katika upya wa uzima. Kwa maana kama mlivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika mtaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake; mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulubishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena; kwa kuwa yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi…” (Rum.6:1-7)
“Maana kwa kule kufa kwake, aliifia dhambi mara moja tu; kwa kule kuishi kwake, amwishia Mungu. Vivyo hivyo ninyi nanyi jihesabuni kuwa wafu kwa dhambi na wlaio hai kwa Mungu katika Kristo Yesu. Basi dhambi isitawale ndani ya miili yenu ipatikanayo na mauti, hata mkazitii tamaa zake; wala msiendelee kuvitoa viungo vyenu kuwa silaha za dhuluma kwa dhambi; bali jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai baada ya kufa, na viungo vyenu kwa Mungu kuwa silaha za haki. Kwa maana dhambi haitawatawala ninyi, kwa sababu hamwi chini ya sheria, bali chini ya neema.” (Rum.6:10-14)
Mpendwa msomaji wangu, maandiko tuliyonukuu hapap juu, yameweka waziwazi “nafasi ya dhambi” ya dhambi katika ulimwengu wa sasa, hususan katika miili yetu hii hii ya mauti! Ukihesabu katika mistari hii utakuta neno “dhambi” limetajwa mara kumi na moja. Katika hizo kumi na moja ziko sehemu tano ambapo dhambi imetajwa kama kitu kisicho na nguvu tena, na kama kitu kisichostahili kutawala tena katika maisha yetu. Hebu nikupitishe kwa haraka maandiko hayo kama ifuatavyo:
a)    “…sisi tuliofia dhambi tutaishije tena katika dhambi?...” Tafsiri ya maandiko haya maana yake ni “Kuwa ndani ya Kristo” maana yake ni “kutengwa mbali na dhambi”; na kwamba kuendelea katika dhambi wakati umo ndani ya Kristo ni kinyume kabisa na kazi ya Yesu iliyofanyika msalabani!
b)    “…..utu wetu wa kale ulisulubishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena;…” Tafsiri ya maandiko haya maana yake ni: Wakati Yesu alipokuwa juu ya msalaba, utu wetu wa kale, kwa wakati huo huo ulihukumiwa juu ya mwili wa Yesu. Kwa tukio hilo, makali ya dhambi yaliyokuwa yametawala katika miili yetu yakavunjwa nguvu zake. Na kwa kila mtu atakayempokea Yesu Kristo nguvu ya dhambi ibatilike katika maisha yake; na asiendelee kutumikishwa kwa mabavu na nguvu ya dhambi!
c)    “…..jihesabuni kuwa wafu kwa dhambi na walio hai kwa Mungu katika Kristo Yesu…” Tafsiri ya maandiko haya maana yake ni: walioko ndani ya Kristo, wajitambue kwa imani, kwamba kwa habari za maisha ya dhambi wao wamekufa. Na badala yake utu mpya, tabia mpya za kiungu view hai, na kuonekana kwa uhalisi mbele za Mungu
d)    “….dhambi isitawale ndani ya miili yenu ipatikanayo na mauti, hata mkazitii tamaa zake…”  Tafsiri ya maandiko haya maana yake ni kwamba, tunatangaziwa na kutahadharishwa, kuwa makini kutokuiruhusu, au kuipana nafasi dhambi iendelee kutawala kwa sababu ya vishawishi vitokanavyo na majaribu ya tamaa za mwili.
Kimsingi, hapa inaonekana kwamba, japokuwa dhambi yenyewe kama dhambi kiuhalisia, haina tena nguvu ya kutawala katika miili yetu; lakini upo uwezekano kwetu sisi wenyewe; kwa mtazamo wetu tu kuiruhusu, kuifungulia dhambi milango ya maarifa ili irudi na kutawala kama hapo awali. Ikitokea hivyo, kwa mujibu wa maandiko haya, itambulike kwamba “sio maisha mapya ya ushindi dhidi ya dhambi yaliyokusudiwa ndani ya Kristo” ; bali kwa mtazamo wetu tumeifufua dhambi kurejea na kuendelea kutawala katika mwili wake.
e)    “…Kwa maana dhambi haitawatawala ninyi,…” Tafsiri ya maandiko haya maana yake ni kwamba, dhambi haitatutawala. Maana yake ni ile ile ikiwa imerejewa tena na tena, ya kwamba dhambi haipaswi na haina nguvu za kututawala.
Kielelezo cha imani cha kuvunja
nguvu ya dhambi katika miili yetu

Baada ya kupata ushahidi wa kubatilishwa kwa nguvu ya dhambi isiendelee kutawala tena katika miili yetu; naomba sasa tupitie kwa ufupi kielelezo cha imani, kilichoamriwa na Yesu Kristo mwenyewe na kutekelezwa na mitume wake. Kielelezo hicho ni Toba na ubatizo!
Tukumbuke Yesu Kristo mwenyewe baada ya kufufuka kwake aliwatokea wanafunzi wake na kuwaagiza kwamba, wakaihubiri Injili ya ukombozi, na kila atakaiamini itamlazimu kutubu (kubadili mtazamo kuhusu nafasi ya dhambi;) na kuiruhusu kazi ya ukombozi wa Kristo ifanyike halisi katika  maisha yake. Maana ya Yesu kuagiza ubatizo, ni kwamba hii ndiyo njia pekee ya kuonesha mfano wa kifo, mazishi na ufufuo wa Kristo katika maisha ya kila anayemjia Yesu kwa imani.
Kwa kuwa tendo la ubatizo ni tendo la kuzamisha, kuzika mtu ndani ya maji mengi, Yesu aliliagiza liwe kielelezo cha kifo  mazishi na kufufuka kiroho na hatimaye kufufuka kimwili siku ya kiyama. Sasa basi, tukirejea kwenye maandiko yetu yale yale Warumi. 6:1-7; 10-14; tunakwenda kuthibitisha jinsi kielelezo cha toba na ubatizo kilivyo na uhusiano wa kiimani na mchakato mzima wa Kusulibishwa, kufa na kufufuka kwa Yesu Kristo..
a)    “…Yesu aliposulibiwa msalabani……”  maana yake “…utu wetu wa kale ulisulubishwa pamoja naye”
b)    “…Yesu alipokufa msalabani……”  maana yake “…tuliifia dhambi juu ya mwili wa Yesu”
c)     “Yesu alipozikwa….” Maana yake “…Tulibatizwa katika mauti yake….” Na “…Tulizikwa pamoja naye  kwa njia ya ubatizo katika mauti yake…”
d)    “Yesu alipofufuka katika wafu…” maana yake “…tuenende katika upya wa uzima…”
e)    Kuishi kwake Kristo mbele za Mungu maana yake “miili yetu isitumikie dhambi tena…”
Majumuisho
Tumejifunza kwamba, kazi aliyofanya Yesu Kristo msalabani ilikuwa ni kuivinja nguvu ya dhambi isipate kutawala katika miili yetu ya mauti na tuishi maisha ya ushindi dhidi ya dhambi katika ulimwengu huu wa sasa. Aidha, tumejifunza pia kwamba dhambi kuendelea kutawala katika ulimwengu wa sasa na katika miili ya binadamu wa leo; sio kwa sababu bado ina nguvu kama kablal Yesu hajasulibiwa msalabani; bali ni kutokana na “kutokubadili mtazamo wetu kuhusu nafasi ya dhambi ulimwenguni, na kwamba kwa njia hii,, tunaipa dhambi nguvu sisi wenyewe, na inatawala kwa ridhaa yetu! Kisha tumeshuhudia kwamba toba na ubatizo ni kielelezo cha imani kinachoifanya kazi ya Kristo iwe halisi katika maisha ya kila anayemwamini.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni