Ukiheshemiwa heshimika
Utangulizi
Leo nimeona niwasilishe
makala ambayo ni kutathimini hali halisi ya tabia na mwenendo wa kila mtu
binafsi pamoja na jamii kwa jumla. Na kitu ambacho natamani tukifanyie tathmini
kwa kila mmoja wetu ni msamiati wa neno maalum lijulikanalo kama “heshima”!
Nataka tulitafakari neno heshima katika maana zake na matumizi yake na
kuchunguza ni kwa kiasi gani viwango vyake vinazingatiwa katika jamii ya kizazi
hiki.
Na kabla ya kuanza
kulitathmini, hebu kwanza tupate tafsiri yake pamoja na matumizi yake asilia. Kwa
mujibu wa tafsiri ya Kiswahili sanifu, tunapata maana ya neno “heshima” katika
maelezo kama ifuatavyo: 1. Thamani ya utu, utukufu, daraja la juu; 2. Staha,
adabu, nidhamu; 3. Kitu anachopewa mtu Kama alama ya kuthaminiwa kwake
Msomaji mpenzi, ukifuatilia
kwa makini maana ya “heshima” kwa kupitia maneno yaliyoainishwa hapa juu,
unaweza kuigawa “heshima” katika aina kuu mbili za sifa. Aina ya kwanza ni “sifa za nje” na aina ya
pili ni “sifa za ndani.”
Aina ya kwanza ya heshima ya
“sifa za nje” ndiyo inayosababisha wahusika kuonekana kuwa na “thamani ya utu”,
au “utukufu” au kuwa katika “daraja la juu”. Mambo haya matatu ndiyo humfanya
mtu “kujulikana na wengi katika jamii” (Public figure) au “kuwa maarufu”
(famous). Kimsingi “kujulikana” na wengi na kuwa “maarufu” ndiko humfanya
mhusika kupata “heshima ya hadhara” (reputation)
Kwa maelezo mengine, “sifa za
nje” ni mambo ambayo muhusika amefanikiwa
kuyafanya baada ya kujipatia elimu, ujuzi na kufikia utendaji wa viwango vya ubora
vinavyotambulika na mamlaka husika. Kwa
kifupi, “sifa za nje” hutokana na “mafanikio ya nje” na kumfanya mtu
kuheshimiwa katika jamii.
Aina ya pili ya heshima ni
sehemu ya “sifa za ndani” ambayo hutokana na “staha”, “adabu” na “nidhamu” Haya
mambo matatu yanahusu tabia na mwenendo wa mtu binafsi kwa jinsi anavyohusiana
na watu wengine wanaomzunguka.
Hizi “sifa za ndani” ndizo
zinazo muwezesha muhusika baada ya kupata mafanikio ya “kujulikana” na kuwa
“maarufu” kuendelea kujistahi na kustahi wengine, kuwa na adabu na nidhamu
binafsi.
Hizi ni “sifa za ndani”
ambazo hujenga tabia binafsi ya uadilifu na uaminifu na kuendelea kutunza
heshima ambayo ni “thamani ya utu”, “utukufu” na “daraja la juu” katika jamii
Vyanzo vya heshima
Msomaji mpenzi, kama tulivyokwisha kujifunza tafsiri ya msamiati wa neno “heshima”; tumeshuhudia kwamba yako mambo maalum ambayo ni chimbuko na vyanzo vya heshima. Mpaka mtu afikie kiwango cha “kuheshimiwa” mbele ya jamii, lazima awe amefanya mambo na kuonesha ufanisi unaozingatia viwango vya ubora. Baadhi ya mambo ambayo ni vyanzo vya mtu kuheshimiwa katika jamii ni pamoja na:
Msomaji mpenzi, kama tulivyokwisha kujifunza tafsiri ya msamiati wa neno “heshima”; tumeshuhudia kwamba yako mambo maalum ambayo ni chimbuko na vyanzo vya heshima. Mpaka mtu afikie kiwango cha “kuheshimiwa” mbele ya jamii, lazima awe amefanya mambo na kuonesha ufanisi unaozingatia viwango vya ubora. Baadhi ya mambo ambayo ni vyanzo vya mtu kuheshimiwa katika jamii ni pamoja na:
1.Kipaji cha
uongozi wenye ushawishi mkubwa katika utawala na utumishi wa umma
2.Kipawa cha kiroho
katika utumishi wa mambo ya dini
3.Elimu ya juu na
ujuzi wa kitaaluma
4.Hekima na uwezo
wa kumiliki mali na utajiri
5.Vipaji maalum vya
sanaa na michezo
Japokuwa vinaweza kuwepo
vyanzo vingine zaidi katika kumfanya mtu “kuheshimiwa” mbele za jamii, lakini
mambo haya matano niliyoyataja yamebeba uzito wa juu na uchambuzi wangu
utalenga haya.
Tunao watu waitwao
“waheshimiwa” kutokana na juhudi katika kujipatia elimu na ujuzi wakafanikiwa
kupanda madaraja ya kitaaluma na hivyo wakajulikana na kuwa maarufu na hivyo
“wakaheshimiwa” na jamii.
Tunao wengine ambao kupitia
vipaji vya uongozi walivyojaliwa katika utumishi wa umma na kwenye madhehebu
yetu ya dini, wamejikuta wamejulikana na kuwa maarufu na wanaitwa “waheshimiwa”
kwa misamiati ya majina ya vyeo na madaraka waliyonayo katika jamii
Tunalo pia kundi la baadhi ya
watu ambao wamejaliwa hekima na uwezo wa kufanya shughuli za za uzalishaji mali
na kumiliki utajiri ambao umewafanya kujulikana na kuwa maarufu na jamii
imewaheshimu kwa sababu hiyo.
Kana kwamba hii haitoshi,
tunalo kundi la wenye vipaji vya sanaa na michezo ambao wameonesha uwezo na
ubunifu na umahiri katika tasnia za burudani mbalimbali na kujikuta
wamejulikana na kuwa maarufu, na kupata heshima mbele za jamii inayowazunguka.
Hawa wote, wamejulikana na
kuwa maarufu, kupitia vyanzo nilivyovitaja, wakapokea heshima kuliko watu
wengine.
Tishio la kujivunjia heshima
baada ya kuheshimiwa
Hapo mwanzo tumekwisha
kuigawa heshima katika aina kuu mbili za sifa za nje na sifa za ndani. Bila
shaka tunaweza kujiuliza ni “Heshima” ipi iliyo bora? Ni sifa za nje au sifa za
ndani? Kwa tathmini naweza kusema kwamba “ubora wa heshima” ni muunganiko wa “sifa
za nje” na “sifa za ndani”.
Hakuna “ubora wa heshima”
unaotegemea sehemu moja pasipo nyingine. Heshima ya umaarufu na kujulikana
hudumu tu iwapo wahusika watazingatia
tabia za kujistahi, adabu na nidhamu binafsi mbele za watu
wanaowazunguka.
Hata hivyo, kwa bahati mbaya,
watu wengi wenye kupata heshima zitokanazo na sifa za nje, baada ya muda si
mrefu sana hujikuta wanapoteza heshima zao mbele ya jamii. Na hata kama wahusika
bado wanaendelea kujulikana na kuwa maarufu kwa kutegemea sifa za nje; lakini wanapoacha
kujistahi, kuwa na adabu na nidhamu binafsi, tayari hupatwa na mmomonyoko wa
maadili ambao huathiri “thamani ya utu” wao, na kuutia dosari umaarufu wao; na
hata kudhalilisha “madaraja ya juu” waliyokwisha kujipatia mbele za jamii
Heshima ya mtu ili iwe
endelevu, lazima ijengwe juu ya "sifa za ndani" ambazo hutokana na
mtu kujizoeza katika mambo ya "staha, adabu na nidhamu" mambo haya
ndiyo humjengea mtu tabia ya uadilifu na uaminifu!
Kwa bahati mbaya "waheshimiwa" wengi hutoa kipaumbele kwa "sifa za nje" ili kutengeneza umaarufu (reputation); na kisha kupuuza uboreshaji wa "sifa za ndani" za "staha”, “adabu”, na “nidhamu"; ambazo kimsingi ndizo huifanya heshima kuwa bora (integrity)
Itaendelea
toleo lijalo,
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni