Ama kweli Wahenga walisema; “duniani kuna mambo.” Jamaa mmoja
aliyejiita ‘mungu’ huko nchini Kenya, Jehova Wanyanyi amefariki duniani na
kuacha wake 35 na watoto zaidi ya 95.
Wanyonyi alizaliwa mwaka 1924 magharibi mwa Kenya, karibu na Mlima
Elgon ambako anatambuliwa kama Mlima Sayuni.
Wanafamilia na waumini wa kiongozi huyo wa dini aliyoianzisha na
kuiongoza, wanasisitiza kuwa ‘mungu’ wao bado yupo hai, ingawa uongozi wa Serikali
ya kijiji alichokuwa akiishi unasema Wanyanyi alifariki dunia Julai 18 mwaka
huu.
Taarifa za kufariki dunia kwa Wanyanyi zilianza kusambaa tangu Julai
mwaka huu, lakini ndugu zake walikuwa wakisisitiza kuwa mungu wao hajafa na
kwamba hakuna mwenye mamlaka ya kuhoji mahali alipo.
Baadhi ya viongozi katika eneo alilokuwa akiishi Wanyonyi wanasema
kuwa ‘mungu’ huyo alifariki dunia akiwa njiani kupelekwa katika Hospitali ya
Kitale baada ya kuzidiwa.
“Wanafamilia walikuja kwangu kuomba kibali cha mazishi, baada ya
aliyejiita Jehova Wanyonyi kushikwa na ugonjwa akiwa njiani kwenda Cherangany
Nursing Home Kitale mjini,” alisema Chifu Kipsomba Daniel Busienei
alipozungumza na gazeti la The Standard la Kenya.
Chifu Busienei alisema wanafamilia walikwendea kumwomba kibali ya
mazishi ili waende hospitali wakachukue mwili wa Wanyonyi kwa kuwa
wasingekabidhiwa maiti hiyo bila ya kuwa na kibali hicho.
“Nilimwambia msaidizi wangu awape kibali, waende wakampumzishe
Wanyonyi,” alisema Chied Busienei.
Msaidizi wa chifu, Paul Bett anathibitisha kuwa alitoa kibali kwa
familia hiyo Julai 19, siku moja baada ya uvumi kuenea kuwa Wanyonyi amefariki
dunia.
“Alifariki dunia Julai 18, akiwa njiani kuelekea hospitali na kijana
wake ndiye aliyekuja kuomba kibali siku iliyofuata,” alisema Bett.
Wiki mbili zilizopita vyombo vya habari vilizuiliwa kuingia katika
makazi ya Wanyanyi yaliyopo katika Kijiji cha Chemororoch, Jimbo la Soy kwa
maelezo kwamba ‘mungu’ wao alikuwa mzima wa afya.
Waandishi hao walifika katika eneo hilo baada ya kupata
taarifa kuwa Wanyonyi amefariki dunia. Baadhi ya wanafamilia wakiwamo watoto na
wake zao, walisema kuwa mungu wao mwenye enzi alikuwa salama.
Awali, ilielezwa kuwa Jehova amelazwa katika Hospitali ya Cherangany
kabla ya kusafirishwa kwenda katika Hospitali ya Rufaa ya Moi huko Eldoret.
Hata hivyo, utata wa kifo hicho uliongezeka baada ya waandishi wa
habari kushindwa kuliona jina la ‘mungu’ huyo katika orodha ya majina ya watu
waliokuwa wamehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti.
Utata wa kifo cha mungu huyo aliyekuwa kiongozi wa huduma ya Lost
Israelites of Kenya, yenye wafuasi wengi katika mpaka wa majimbo ya Uasin Gishu
na Kakamega, ulichochewa na maoni tofauti yaliyokuwa yakitolewa na watu
mbalimbali.
Msemaji wa familia ya kiongozi huyo, Eliab Masinde aliendelea
kukanusha kuwa mauti imemchukua mungu wao, licha ya uongozi kuthibitisha kifo
hicho.
Masinde alisema: “Jehova ni mzima, ingawa hali yake si nzuri sana,
amelazwa katika moja ya hospitali jijini Nairobi akipatiwa matibabu kwa
usimamizi wa watoto wake wawili.”
“Alikuwa na maumivu ya mgongo kwa muda mrefu, lakini alipelekwa
hospitali na watoto wake huko Nairobi. Mungu huwa hafi, kama angekuwa amekufa,
tungeshapata taarifa,” alisema Masinde.
Msemaji huyo wa familia ambaye pia ni mwangalizi wa madhabahu wa
huduma hiyo, alisema majirani wa Wanyonyi waliomwona alipokuwa akipelekwa
hospitali ndio walioeneza uvumi wa kifo chake.
Mkazi mmoja wa kijijini hapo, ambaye hakutaka kutaja jina kwa
kuihofia familia ya mungu huyo, alisema kiongozi huyo alifariki ingawa
wanafamilia wanaficha suala hilo.
“Jehova alikuwa ana maumivu ya mgongo kwa muda mrefu, alikuwa
anatembelea kiti cha magurudumu kabla hajatoweka. Alikuwa ni mzee na
tunachokijua, familia inatawa kumweka mrithi wake kwa siri,” alisema.
Anaongeza kuwa Jehova ana wafuasi wengine nchini Uganda na kwamba
inawezekana mwili wake umepelekwa huko kwa ajili ya mazishi.
Tangu taarifa za kifo hicho kutolewa, waumini wengi wamekuwa
wakifika nyumbani kwa kiongozi wanayemtaja kuwa ni ‘mungu aliye hai’ kumwombea
ili apate nafuu haraka.
Baadhi ya wananchi wamekuwa na maoni tofauti kuhusu kifo hicho, huku
wengine wakisema haiwezekani mungu kufariki dunia.
John Paul alisema kupitia mtandao kuwa: “Inakuwaje mungu akafa au
kuugua? Kama kweli alikuwa mungu, hakupaswa hata kuugua, achilia mbali kifo.”
Wanavyoabudu
Waumini wa Wanyanyi, husujudu mbele yake na kuomba wanachotaka.
Mwandishi wa BBC, Muliro Terewa aliingia katika kanisa hilo na kumsikia muumini
akisali:
“Mungu mkuu, uliyekuwepo, upo na utakuwepo Jehova. Wewe ndiye
aliyezungumzwa kwenye Biblia katika Kitabu cha Isaya 11. Tunakuheshimu kwa
sababu kama ulivyosema mwisho umekaribia, tunaomba utuongoze kwenda mbinguni.”
Akihojiwa na BBC, Wanyonyi alisema:”Mimi ni masikini nina watoto 95
wa kuwalisha. Waangalie watoto hawa, hawajala kitu chochote asubuhi hii,
nahitaji dola 13 (Sh26, 000) niwanunulie mikate.”
‘Mungu’ huyo alisema aliingia kwenye mwili wa mwanadamu miaka mingi
iliyopita kama ilivyoandikwa katika vitabu vitakatifu.
Aliongeza: “Jehova nilimtuma mwana wangu kuwaokoa watu wake lakini
wanakataa, hivyo nimeamua kuja mwenyewe labda watu wanaweza kuacha uovu wao.”
Alihadharisha kuwa kama hawatakubali na kubadilika, ataagiza moto kutoka
mbinguni uwachome, lakini wanaoamini kuwa yeye ni mungu hawataungua.
Waumini wa Wanyanyi wanasema wameshuhudia ‘mungu’ wao akifanya
miujiza, ukiwamo ule wa mume na mke waliokuwa wakiugua Ukimwi kupona kabisa.
Hata hivyo, wakati waumini wake wakipaza sauti kuwa Wanyonyi ni
‘mungu’, baadhi ya watu walitishia kumuua iwapo wangemtia mikononi mwao.
“Wanyonyi ni nabii wa uongo. Ni miongoni mwa manabii wa uongo
waliosemwa kwenye Biblia,” alisema Mchungaji Julius Makona.
Patrick Busolo alisema: “Wanyanyi siyo Mungu, anajikusanyia mali tu
kwa kutumia imani aliyowajengea waumini wake. Anawalazimisha watu wamfanyie
kazi ili aweze kuishi vizuri.”
Wanyanyi alisema kuwa aliuteremsha Ukimwi duniani kama adhabu kwa
wanadamu wanaodharau amri za Mungu.
Wakati ikithibitika kuwa ‘mungu’ Wanyanyi amefariki dunia, kazi
iliyobaki ni kwa waumini wake kumteua kiongozi mwingine atakayesimamia mamia ya
waumini wa dhehebu hilo.
Pia, itakumbukwa kwamba, ‘mungu’ huyo alikuwa akisisitiza kwamba
hakuna Mungu mwingine isipokuwa yeye pekee aliyeumba vitu vyote. Kiongozi ajaye
atasema ametoka wapi?
Bila shaka jibu wanalo waumini wa The Lost Israelites, wanaoomboleza
kifo cha ‘mungu’ wao.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni