YESU NI JIBU

Jumatano, 31 Oktoba 2012

NAMNA YA KUMSIFU NA KUMWABUDU MUNGU--MWALIMU MGISA


Tumejifunza mambo mengi sana yaliyokuhamasisha na yaliyokupiga deni uwe
kiumbe wa kumsifu na kumtukuza Mungu. Tunapomsifu mtu, huwa
tunaelezea yale ambayo yanamtofautisha na wengine. Hivyo basi, ufikapo
katika muda wa kumsifu na kumwabudu Mungu, ujue namna ya kuifanya sifa
yako na ibada yako kwa usahihi.  
                   
Na ili kumpa Mungu sifa na ibada, ni lazima na ni muhimu sana ujue
mambo ambayo yanamstahilisha Mungu wetu kusifiwa na kutukuzwa. Kwa
kutumia sifa na tabia za Mungu, utaweza kumsifu na kumwabudu vizuri.
Hakuna kiumbe kingine chochote kinazo zile sifa kuu tano za Mungu,
isipokuwa yeye Mungu Jehova peke yake.  
                    
Kwahiyo, na hizo ndizo zinayomstahilisha yeye kusifiwa na viumbe
wake. Katika sura ya nane, tumeshajifunza mambo yanayomstahilisha Mungu
kupewa sifa. Kwakuwa sasa unayajua, basi tumia mambo hayo uendapo
mbele za Mungu katika katika ibada yako ili kumsifu na kumwabudu.
Unapomueleza Mungu sifa zake na tabia zake (vile alivyo) hapo unakuwa
unamsifu na kumwabudu.

Tofauti ya kusifu na kuabudu
Naomba urudie kuisoma sura ya kwanza ya kitabu hiki, ambapo nimefundisha
vizuri maana ya kumshukuru Mungu, kumsifu Mungu na kumwabudu Mungu.
Hii itakusaidia kutofautisha mambo haya kwa nia ya kuyaelewa au kuyaelezea
kwa mtu mwingine. Nilisema hivi,  
Ibaba ni kitendo cha mtu kumtukuza, kumhimidi, kumwinua, kumwadhimisha,
kumshukuru na kumheshimu Mungu kwa vile alivyo na kwa yale aliyoyatenda.
(Appreciation and admiration for who God is and for what He has done).
Lakini haya mambo matatu, yanayofanana sana na si rahisi sana
kuyatenganisha kimaelezo au kivitendo.
                
Lakini tuendapo mbele za Mungu kwa ibada, iwe ni chumbani kwako
au sebuleni kwako au kwenye gari lako au kanisani kwako, kusifu na kuabudu
na kushukuru, ni mambo yanayofanyika kwa kuingliana sana. Sio sheria
kwamba, hautakiwi kuchanganya sifa na kuabudu na kushukuru, hapana.
Hebu soma tena sura ya kwanza vizuri. Kati ya mengi, nilisema hivi;
                
Haya mambo matatu, kusifu, kushukuru na kuabudu, ni mambo
yanayofanana sana. Inaweza ikawa vigumu kidogo kuyatenganisha kimaelezo
au kivitendo. Ni ngumu kidogo, kufanya kimoja pasipo wenzake, kwasababu ni
mambo yanayokwenda kwa pamoja sana. Lakini kwa tafsiri zake, yako hivi;
1. Kumshukuru Mungu;‐  Ni ile hali ya kumueleza Mungu jinsi
tunavyothamini (Appreciate and Admire) wema wake, fadhili zake na
baraka zake katika maisha yetu.
2. Kumsifu Mungu;  ‐ Ni kumueleza Mungu juu ya matendo yake makuu
na ya ajabu aliyoyafanya. Au ni kuwaeleza wengine kuhusu matendo
makuu ya Mungu aliyoyafanya katika maisha yetu au kwa watu
wengine.
3. Kumwabudu Mungu; ‐ Ni kumueleza Mungu tukuzo zetu, heshima yetu
na upendo wetu kwake kwasababu ya uzuri wa tabia zake kwetu.
(Credentials and Characters).   
Kwahiyo, tuendapo mbele za Mungu kwa ibada, iwe ni chumbani kwako au
sebuleni kwako au kwenye gari lako au kanisani kwako, ili kumsifu na
kumwabudu na kumshukuru Mungu, uwe huru kujimimina mbele za Mungu
kwa kufanya vyote vitatu, kwa namna moyo wako utakavyokuwa unaongozwa
na Roho Mtakatifu. Vyote vitatu vinatengeneza ibada takatifu kwa Mungu.
                Katika sura inayokuja, nimefundisha vizuri namna ya kuingia katika
ibada na hata kupenya na kufika katika chumba cha ndani kabisa cha uwepo
na utukufu wa Mungu; ili unapokwenda mbele za Mungu wetu, uweze
kukutana na nguvu zake katika utukufu wake.  
                
 Lakini hapa chini nimeziweka kwa ufupi ili kukukumbusha. Na pia
nimekuongezea na mambo mengine yanayotakiwa katika kumsifu na
kumtukuza Mungu. Kwahiyo, utengapo muda wa kukaa mbele za Mungu wetu
kwa ibada, msifu na kumtukuza Mungu kwa mambo yafuatayo,
1. Mtukuze Mungu kwa Sifa zake za Uungu (ambazo hakuna mwingine
aliye nazo) Kwamba;
a) Jehova ni Mungu wa Milele
b) Jehova ni Mungu Mtakatifu
c) Jehova ni Mungu Aliye kila mahali
d) Jehova ni Mungu Anayejua mambo yote
e) Jehova ni Mungu Aliye na nguvu zote na    
      anaweza kufanya mambo yote kabisa.
Nimezielezea vizuri hizi sifa za Uungu, katika sura ya kwanza. Hizi ni baadhi tu
ya sifa za Mungu, sio zote. Kwa hivyo basi, pamoja na namna nyingine ambazo
utajifunza kumsifu na kumwabudu Mungu, hebu uwe unamsifu Mungu kwa
mambo haya au kwa sifa zake hizi pia.  
Msifu Mungu kwa;  
2. Kwasababu ya Tabia zake
3. Kwasababu ya Matendo yake ya Ajabu
4. Kwasababu ya Fadhili nyingi na kuu mno
5. Kwasababu ya Ahadi zake kubwa za thamani2.   Mtukuze Mungu  kwa Tabia zake
Neno la Mungu, linatuonyesha jinsi ambavyo Mungu wetu ana tabia na
kawaida nyingi nzuri ambazo kwa hizo, tunavutiwa na tunapigwa deni kumsifu
na kumwabudu. Kwa mfano ; Biblia inasema kwamba, Mungu wetu amejaa
Upendo, usio na mwisho. Ni Mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira, sifa
yake ni kuwa na rehema daima. Soma mistari ifuatayo, ili uone zaidi. Lakini
kwasababu ya sifa hizi (Tabia zake), tunapigwa deni kumsifu na kumwabudu.
*Zaburi 103:8, Kutoka 34 :6,  
*Efeso 3 :18‐19, Daniel 9 :4, Ufunuo 19 :11
3. Mtukuze Mungu  kwa Matendo yake ya ajabu.
Mungu wetu ni Mungu aliyefanya mambo ambayo hakuna tena, awezaye
kufanya. Kwa mfano; ndiye aliyeziumba na kuzitundika sayari zote za
ulimwengu huu, bila minyororo wala nguzo. Mungu wetu ndiye
anayesababisha mioyo yetu inadunda, bile kuwekewa betrii wala chaji
(charge). Au ni lini ulichomeka moyo wako katika soketi ya umeme kama
unavyochomeka simu yako ili kupata umeme?
       
 Nina uhakika, hakuna mtu anayefanya hivyo. Sasa unadhani moyo
wako unadundaje? Hizo ni kazi za ajabu za Mungu wetu.na hakuna mtu
awezaye kuzifanya. Kwasababu ya matendo yake ya ajabu, Mungu wetu
anastahili kusifiwa na kutukuzwa. Soma mistari ifuatayo kwa umakini.
Utaweza kuona kwa uchache, jinsi maandiko yanavyoeleza juu ya matendo
makuu ya Mungu.  
Haya ni maelezo ya watu wa Mungu ambao kwa kumjua Mungu, waliweza
kueleza ukuu wake vizuri, ili na sisi tunaosoma maandiko yao, tunajifunza juu
ya ukuu wa Mungu, uweza wa Mungu na tabia za Mungu wetu. Soma vizuri
Kitabu cha Daniel 6:25‐27,  Nehemia 9:6,  Zaburi 147:1‐18,  na Zaburi sura ya
136:4‐26
4. Mtukuze Mungu  kwa Fadhili zake.
Mungu wetu ni Mungu atupaye baraka na fadhili nyingi kila siku. Fikiri wema
ambao Mungu amekufanyia maishani mwako, na hata katika siku ya leo tu.
Kuna vingi ametupa ambavyo wengi walitamani, lakini hawakupewa. Uhai,
afya, ulinzi, rehema, chakula, fedha, shule, simu, gari, nyumba, ajira, mke,
mume, watoto, na hata wazazi.
                  Sio kila mtu bado ana wazazi. Na wengine wamezaliwa hawajawahi
kuwajua wazazi wao. Kwakweli fadhili na baraka za Mungu ni nyingi sana;
ukiamua kuziorodhesha, utakesha. Sasa, kwa fadhili zote hizi alizotujalia, basi
Mungu wetu anstahili kusifiwa.
*Zaburi 103:1‐5,  Zaburi 107:21,  2Nyakati 20:21
5. Mtukuze Mungu  kwa Ahadi zake.
Ni Mungu aliyetuahidi watu wake, mambo mengi sana mazuri. Ametupa ahadi
kubwa mno na za thamani sana. Ni ahadi za kutupa baraka, heshima na utajiri.
Kwa ahadi hizi pia, anastahili kusifiwa * 2Petro 1:3‐4,  Efeso 1:3‐4,  Kumbu 4:4‐
      8  Kwa ufupi, hivi ndivyo unavyotakiwa kumsifu na kumwabudu Mungu.
Kadri unavyoanza kufanya hivi kwa vitendo, utaendelea kujifunza kufanya
huduma hii ipasavyo, nawe utajikuta unakutana na nguvu za Mungu kwa
namna ya tofauti maishani mwako.
                              MSIFU MUNGU KWA MAJINA YAKE.
Majina ya Mungu, hueleza sifa za Mungu, Tabia za Mungu au Matendo ya
Mungu. Mfano; Wayahudi wanamwita Mungu El‐Shaddai. Ni neno lenye
majina mawili ndani yake. ‘El’ maana yake Mungu, na ‘Shaddai’ lenye maana
itokanayo na neno ‘Shad’ yaani Titi (Ziwa) la mama anyonyeshaye.  
        Kutokana na ukweli kwamba, titi/ziwa la mama anyonyeshaye,
linampa mtoto mchanga kila kitu anchohitaji. Maziwa ya mama yake, humpa
mtoto kila kitu mtoto anachohitaji. Ndani ya maziwa kuna vitamini, protini,
wanga, mafuta, madini, maji, na kila kitu mtoto anachohitaji. Maziwa ya
mama, yanamtosheleza mtoto kwa kila kitu. Hivyo, Waisraeli wanapomwita
Mungu El‐Shaddai, wanamaanisha kuwa, kama ziwa linavyo mtosheleza
mtoto, vivyo hivyo, Mungu ni ‘Mtoshelezi’ kwetu. Halleluyah!
       Hivyo, kila jina la Mungu, linabeba aidha Sifa yake au Tabia yake au
Matendo yake. Ndio maana Mfalme Daudi anasema  
“Mpeni Bwana, enyi wana wa Mungu … Mpeni Bwana utukufu kwa
jina lake. Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu.” (Zab 29:1‐
2) Msifuni Bwana kwa kuwa Bwana ni mwema, Liimbieni Jina
lake, kwakuwa lapendeza.(Zaburi 135:3).
Na Bwana Yesu alitufundisha kuanza sala namna hii;
Baba yetu uliye mbinguni, jina lako tukutuzwe, hakafu Ufalme
wako uje hapa duniani.  
Kwahiyo, unaweza pia kumsifu Bwana kwa majina yake. Majina ya Mungu,
hueleza aidha sifa za Mungu au tabia za Mungu au Matendo makuu ya
Mungu. Yafuatayo hapa chini, ni baadhi ya majina ya Mungu kwa lugha ya
Kiebrania, yatakayokusaidia kumsifu, kumwabudu na kumshukuru Mungu.
                                   
                                           MAJINA YA MUNGU
   
       Jina la Mungu                 Maana yake       Mstari wa Biblia         
1. Adonai ‐ Mungu Mwenye enzi yote ‐ Mwa 15:2‐8, Kut 6:2‐32. El‐Ohim ‐  Mungu Muumbaji       ‐  Mwa 33:20, Kol 1:16‐17
3. El‐Elyon ‐  Mungu Aliye juu zaidi       ‐   Mwa14:18, Dan 4:34
4. El‐Gibbor  ‐ Mungu Mwenye Nguvu    ‐       Isa 9:6,  Zab 147:5
5. El‐Hai ‐  Mungu Aliye Hai/Anaishi   ‐  Josh 3:10,  1Sam17:26
6. El‐Olam ‐  Mungu wa Milele                 ‐  Ufu 4:8,  Kut 3:14
7. El‐Roi ‐  Mungu Aonaye kila kitu       ‐ Mith 15:3, Zab 32:8
8. El‐Shaddai ‐  Mungu Mtoshelezi      ‐  Mdo 17:28, Kumb 8:4
9. Jehovah ‐  Ajitegemeaye kuwepo ‐Kut 6:2‐8,  Mdo 17:24‐25
10. Jehovah Shalom    ‐Mungu Amani yetu           ‐ Amu 6:22‐24
11. Jehovah Rapha   ‐  Mungu Atuponyaye                ‐  Kut 15:26
12. Jehovah Jireh   ‐  Mungu Mtoaji wetu           ‐ Mwa 22: 8, 14
13. Jehovah Nissi  ‐  Mungu Ushindi wetu          ‐ Kut 14:13‐14  
14. Jehovah Saboath  ‐  Bwana wa Majeshi             ‐  Malaki 3:7  
15. Jehovah Shammah ‐  Bwana ni Aliyepo                  ‐  Kut 3:14  
16. Jehovah Rohi   ‐  Bwana  ni Mchungaji wangu   ‐  Zab 23:1
17. Jehovah Tsidkenu  ‐  Bwana ni Haki yetu              ‐  Yer 23:6
18. Jehovah Mekaddishem  ‐  Bwana Atutakasaye  ‐  Kut 31:13  
Namna  za  kumshukuru, kumsifu,  na  kumwabudu Mungu  wetu.
Kwahiyo, katika maisha yetu sisi, kama waumini, tunatakiwa kumpa Mungu
wetu ibada, (kumshukuru, kumsifu na kumwabudu) kwasababu ya mambo
yote hayo niliyoyataja. Tunatakiwa kumtukuza Mungu kwasababu ya sifa zake,
na kwasababu ya tabia zake, na matendo yake na fadhili zake na ahadi zake
kwetu.  
    
  Sasa basi, hapa chini, nimekuwekea njia kuu tatu ambazo unaweza
kumsifu na kumtukuza Mungu kwazo. Utengapo muda wa kwenda mbele za
Mungu, unaweza kutuia njiia kuu zifuatazo; Kumtukuza Mungu kwa,
1. Kumwimbia nyimbo za kumsifu na kuwabudu
2. Kumweleza au kusimulia kwa maneno
3. Kumtolea Mungu sadaka na dhabihu 
 
                                          Wako katika kazi ya Mungu
                                            Mwl. Mgisa Mtebe
                                           +255 713  497  654
                                      mgisamtebe@ yahoo.com
                                          www.mgisamtebe.org

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni